The House of Favourite Newspapers

Mastaa Yanga Kuvuna Milioni 450

0

YANGA kweli mwaka huu wameamua, hawataki kabisa mzaha kwani katika kuhakikisha kuwa wanatwaa ubingwa msimu huu wameweka kiasi kisichopungua milioni 15 katika kila mchezo kama bonus endapo timu itaibuka na ushindi huku kwa upande wa Simba wakiweka milioni 6.8 lakini inaweza ikabadilika kulingana na presha ya mechi.

 

Kwa maana hiyo ukipiga hesabu mwishoni mwa msimu kwa timu 15 ambao zinaunda jumla ya michezo 30 kwa mizunguko yote miwili, wachezaji wa Yanga wanakuwa wamekusanya kiasi kisichopungua milioni 450 huku wachezaji wa Simba wao wakiwa watakusanya kiasi kisichopungua milioni 300.

 

Hivyo kwa maana hiyo, mpaka sasa Yanga baada ya kuibuka na ushindi katika michezo miwili mfululizo ya ligi dhidi ya Kagera Sugar na Geita Gold, wachezaji hao wanakuwa wamekusanya jumla ya milioni 30 huku Simba wachezaji wakiwa wamechota milioni 10 za ushindi dhidi ya Dodoma Jiji.

 

Vyanzo vyetu vya ndani kutoka Simba na Yanga tayari vimelithibitishia Championi Jumatano kuwa, uongozi wa Yanga chini ya wadhamini wa timu wameongeza bonasi ya ushindi katika michezo ya ligi kuu kutoka shilingi milioni 10 za msimu uliopita mpaka milioni 15 ili kuhakikisha kuwa kikosi hicho kinapata matokeo mazuri uwanjani na kwa upande wa Simba wachezaji wao hubeba kiasi kisichopungua milioni 6 na laki nane.

 

“Msimu uliopita bonasi ya timu ikishinda katika michezo ilikuwa ni milioni 10 lakini kwa msimu huu wadhamini wa timu wameongeza na kufikia milioni 15 ili kuongeza chachu ya ushindi katika mechi za ligi kuu, lakini pia bonasi hubadilika kulingana na mchezo husika mfano kwa michezo ile mikubwa kama dhidi ya Simba au Azam bonasi huongezeka,” kilisema chanzo kutoka Yanga.

 

Kwa upande wa chanzo kutoka Simba, kilisema: “Bonasi zimebadilika kwani msimu huu kama timu ikiibuka na ushindi kila mchezaji anabeba laki nne ambapo ukipiga hesabu za wachezaji 17 wanaohusika na mchezo basi wanakuwa wanabeba milioni sita na laki nane lakini pia bonasi zao hupanda na kuongezeka kulingana na ukubwa wa michezo ambayo tunakutana nayo katika ligi kuu.”

 

Alipotafutwa Thabit Kandoro ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Mashindano ya Yanga kuhusu ishu hiyo, aliliambia Championi Jumatano: “Ni kweli bonasi za ushindi ndani ya Yanga zimepanda tofauti na msimu uliopita na hii inatokana na uongozi kuhitaji matokeo mazuri lakini pia bonasi hizi hupanda zaidi kulingana na ukubwa wa timu na uhitaji wa matokeo katika michezo husika.”

Marco Mzumbe na Wilbert Molandi, Dar

 

Leave A Reply