The House of Favourite Newspapers

Mastaa Yanga Wanaitaka Rekodi Hii Msimu Huu

0

ACHANA na bonasi za kila mechi wanazozipata kutoka kwa wadhamini wao kampuni ya GSM imefichuka kuwa kitu kikubwa ambacho kinawapa motisha ya kufanya vizuri mastaa wa Yanga, ni malengo ya kutaka kuandika rekodi ya kushinda ubingwa wa Ligi Kuu Bara baada ya kupita misimu minne.

 

Yanga imeuanza kwa kasi msimu huu kwa kushinda taji la Ngao ya Jamii na kuvuna pointi sita katika michezo yao miwili ya kwanza, huku wakikamatia nafasi ya pili kwenye msimamo wa Ligi Kuu Bara mpaka sasa. Mara ya mwisho Yanga kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara ilikuwa msimu wa 2016/17, na baada ya hapo Simba walitwaa taji hilo mara nne mfululizo.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, aliyekuwa Kaimu Katibu Mkuu ambaye sasa ni Mkurugenzi wa fedha wa Yanga, Haji Mfikirwa alisema: “Miongoni mwa sera za klabu yetu katika kuwapa motisha wachezaji ni kuhakikisha kunakuwepo na kiwango fulani cha bonasi kwa kila matokeo mazuri wanayoyapata, lakini nikuhakikishie kuwa hicho siyo kitu pekee kinachowapa motisha.

 

“Motisha kubwa ambayo wachezaji wote wa Yanga wanayo msimu huu ni ile ya kutaka kuandika rekodi ya kuwa sehemu ya kikosi kitakachorejesha ubingwa wa Ligi Kuu Bara baada ya kupita misimu minne mfululizo bila taji hilo, kila mchezaji anatamani kuona hilo linatimia ndiyo maana wanapambana kufanya vizuri.”

JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply