The House of Favourite Newspapers

Matola Kutua na Silaha Zake Simba

0
Kocha wa Polisi Tanzania, Seleman Matola.

WAKATI kukiwa na tetesi za Kocha wa Polisi Tanzania, Seleman Matola kutakiwa na Simba, taarifa zinasema tayari kocha huyo ameanza kutanguliza silaha zake Mzimbazi.

 

Matola anatajwa kwenda Simba kuwa kocha msaidizi akichukua nafasi ya Denis Kitambi kutokana na klabu hiyo kuwa mbioni kuvunja benchi lake lote la ufundi lililopo chini ya Kocha Patrick Aussems raia wa Ubelgiji.

Kabla ya kutua kikosini hapo, tayari Matola amepanga mikakati yake ya usajili kwa kumuweka ‘stand by’ beki wa kulia wa Namungo, Ally Mohammed Seleman.

 

Taarifa kutoka ndani ya Klabu ya Namungo zinasema kuwa, Matola amekuwa akifanya mawasiliano ya mara kwa mara na beki huyo maarufu kwa jina la Ally Korosho.

Mtoa taarifa huyo aliongeza kuwa, mbali na Matola kumtaka pia beki huyo wa zamani wa Ruvu Shooting, anatakiwa na KMC.

“Matola amekuwa akimuhitaji beki huyu na amepanga katika usajili wa dirisha dogo amchukue. Kama akibaki Polisi Tanzania atamchukua, lakini pia amemwambia ajiandae kwa lolote litakalotokea kwani kuna uwezekano akaenda naye pale Simba.

 

“Baada ya Namungo kucheza na Polisi Tanzania hivi karibuni, Matola alifanya mazungumzo na beki huyo na kuonyesha nia ya kumuhitaji, licha ya kuzungumza pale, lakini pia amekuwa akimpigia simu mara kwa mara. Inaonyesha amemkubali sana.

 

“Si unajua usajili wa dirisha dogo unakaribia, hivyo makocha wengi wanaangalia wachezaji wa kuwasajili, hivyo Matola ameweka rada zake kwa beki huyo lakini pia hata KMC nao wanamuhitaji.

“Ni mchezaji ambaye anategemewa kikosini kwa sasa kwani katika mechi 12 za Namungo msimu huu, amecheza zote,” kilisema chanzo.

 

Beki huyo ambaye mkataba wake na Namungo unatarajiwa kumalizika mwishoni mwa msimu huu, aliweka sawa tetesi hizo kwa kusema: “Nipo tayari kuichezea timu yoyote, si unajua mchezaji kila mmoja na malengo yake, mimi leo nipo hapa, kesho nitakuwa sehemu nyingine, kikubwa naangalia maslahi tu.”

 

Alipotafutwa Matola juu ya hilo, alisema: “Leo (jana Ijumaa) tumewasilisha ripoti yetu katika uongozi wa Polisi Tanzania na kutoa mapendekezo ya nani tumsajili katika usajili wa dirisha dogo. Ni mapema kusema hivi sasa nani tutamsajili.”

 

Jina la Matola ndilo linatajwa zaidi kuchukua nafasi ya kocha msaidizi ndani ya Simba mara tu baada ya benchi hilo kuvunjwa.

Ikumbukwe kuwa, dirisha dogo la usajili hapa nchini linatarajiwa kufunguliwa Desemba 16, mwaka huu na kufungwa Januari 15, mwakani.

 

KITAMBI AMSAFISHIA NJIA

Hata hivyo ishu ya Matola kwenda Simba inaweza ikakamilika muda wowote kuanzia sasa baada ya Kitambi kuomba kwenda kuongeza ujuzi zaidi wa ukocha.

 

Championi linafahamu kuwa, Kitambi ameomba ruhusa hiyo kwa mabosi wa Simba ili akaendeleze taaluma yake na akikubaliwa basi taanza kozi hiyo fupi mara moja huku akiwa anaendelea na majukumu yake kwenye timu.

 

Aidha kocha wa viungo wa timu hiyo, Adele Zrane naye ameomba kwenda kusoma hivyo hii inatengeneza njia zaidi kwa Matola kutua Simba.

Stori na Wilbert Molandi Dar es Salaam

Leave A Reply