The House of Favourite Newspapers

Maumivu Wakati wa Hedhi ‘Dysmenorrhea’

 

Na Dk CHALE| GAZETI LA IJUMAA| AFYA

HALI  hii  hutokea mara tu mwanamke  anapoanza  hedhi yake, huwapata wanawake wengi walio katika umri wa kuzaa na maumivu  huchukua wastani wa siku tatu. Maumivu  huwa  kwenye nyonga hasa upande wa chini wa tumbo. Hali  hii  huambatana  na  maumivu ya kiuno, kuharisha na kichefuchefu.

Kwa wasichana hali  ya maumivu hutokea bila hata ya kuwepo sababu maalumu lakini kwa wanawake watu wazima endapo atakuwa na  maumivu  haya basi lazima kuna tatizo maalum.

Maumivu  ya hedhi kwa wanawake  wenye  umri wa kati ya miaka ishirini na tano wakiwa bado wanapata hedhi husababishwa na uvimbe kwenye kizazi, kuvimba kizazi, hitilafu katika tabaka la ndani la kizazi. Hali  hii  husababisha mwanamke  avurugikiwe na mzunguko wake, kupata damu nyingi sana ya hedhi na kwa muda mrefu na pia huwatokea  wanawake ambao  waliwahi kuvunja ungo kabla ya kufikisha miaka kumi na mbili au kwa wasichana wenye uzito mdogo sana kulinganisha na umri wao, aidha kutokana na kujinyima kula, kukosa lishe bora au kukonda kutokana na  maradhi.

Kwa kawaida, kwa wanawake walio katika umri wa kuzaa na tayari wameshaanza  mahusiano, endapo watakuwa na tatizo hili, basi ni vizuri wafanyiwe vipimo kama Ultrasound mara wanapogundulika na maumivu haya kwa  sababu dalili hizi za maumivu hufanana na matatizo mengine kama la mimba kutunga nje ya kizazi, magonjwa sugu au maambukizi  sugu ya kizazi “PID” na maambukizi sugu ya kibofu cha mkojo. Maumivu wakati wa hedhi huwa hayatokei  sana au yasitokee kabisa kwa msichana mwenye tabia ya kufanya mazoezi ya viungo au kushiriki michezo.

Inashauriwa watoto wa kike wawe na tabia ya kufanya mazoezi kama kukimbia, kucheza mpira, kuruka kamba na mchezo wowote wa kukutoa jasho. Maumivu haya hupungua au kuisha baada ya uchunguzi wa kina na kupata tiba ya dawa za kutuliza  maumivu na dawa za homoni. Endapo kuna tatizo kama uvimbe, basi ni vema mgonjwa  afanyiwe upasuaji kuondoa uvimbe.Kama hakuna tatizo ndani ya kizazi basi maumivu  yataisha taratibu kadiri  utakapoendelea kuzaa.

JINSI TATIZO LINAVYOTOKEA

Maumivu wakati wa hedhi yamegawanyika katika  sehemu kuu mbili. Moja ni Primary Dysmenorrhea
ambapo hapa  mwanamke maumivu yanaanza pale anapovunja ungo na kuendelea nayo na huisha hapo baadaye  anapokuwa mtu mzima.  Pili ni Secondary Dysmenorrhea.

Hapa  mwanamke anakuwa hana historia ya maumivu bali hutokea baadaye na chanzo kikubwa ni hitilafu katika tabaka la ndani, uvimbe ndani ya kizazi,  kuvimba kizazi na uvimbe  wa vifuko vya mayai.

DALILI ZA UGONJWA

Maumivu ya tumbo chini  ya kitovu ndiyo dalili kuu ya tatizo hili wakati wa hedhi. Kwa ujumla dalili zote tumezielezea hapo katika utangulizi. Maumivu  haya ya hedhi huwa yana tabia ya kusambaa kuzunguka kiuno, kulia na kushoto chini ya tumbo. Maumivu makali humfanya mwanamke  ashindwe kuendelea na majukumu mengine na abaki amelala tu nyumbani au amelazwa hospitali.

UCHUNGUZI WA TIBA Hufanyika katika hospitali  za mikoa kwenye kliniki  za madaktari bingwa wa magonjwa ya akina mama. Mgonjwa baada ya uchunguzi wa kina atapatiwa matibabu.

Ni vizuri umuone daktari bingwa wa akina mama kwa uchunguzi. Epuka kutumia dawa bila ya ushauri. Zingatia kufanya  mazoezi ya viungo na  kushiriki michezo.

Kwa stori zote kali, Tu-follow

Facebook @Globalpublishers

Twitter @GlobalHabari

Instagram @GlobalPublishers

YouTube @GlobalTVTZ

Comments are closed.