The House of Favourite Newspapers

Mawaziri Wapya wa JPM Waanika Mikakati Yao, Sasa ni Mchakamchaka

0
Mawaziri na Manaibu Waziri wakiapa, Ikulu Dar.

MAWAZIRI na manaibu walioapishwa na Rais John Magufuli, wametoa ahadi ya jinsi watakavyotekeleza majukumu yao. Mawaziri na manaibu walioapishwa leo Jumatatu wametoa ahadi muda mfupi baada ya kula kiapo Ikulu jijini Dar es Salaam.

Waziri Ofisi ya Rais- Utumishi na Utawala Bora, George Mkuchika amesema atahakikisha watumishi wanakuwepo ofisini kuwahudumia wananchi. Amesema baadhi ya watumishi wamekuwa wakitumia muda mwingi kwenda kunywa chai, hivyo atahakikisha wanabaki ofisini kutoa huduma.

Kuhusu mapambano dhidi ya rushwa, Mkuchika amesema, “Nitatoa elimu na nitatumia muda wangu mwingi na ndugu zangu wa Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa). Nitaongea na Waziri wa Elimu somo la rushwa lifundishwe kuanzia darasa la kwanza hadi chuo kikuu.”

“Ni wizara yenye changamoto nyingi, ng’ombe wanapigwa mnada, hawana maeneo ya malisho, viwanda vya mifugo na mchango wa maziwa ni tatizo, niko katika tafakari, ninajua Rais amenipa changamoto na mimi sijawahi kuchoka na sijawahi kuogopa,” amesema Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhanga Mpina.

Waziri Ofisi ya Rais- Tawala za Mikoa na Serikali za Miata (Tamisemi), Suleimani Jafo yeye amesema, “Tamisemi ni wizara kubwa, niwaombe wakuu wa mikoa, wilaya na watumishi wote wafanye kazi kwa spidi ili tufikie malengo na huduma kwa wananchi.”

Akizungumzia utendaji wake, Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema, “Tutafanya kazi kwa nguvu, jitihada na kasi ili kuhakikisha mifugo na uvuvi inafanikiwa.”

Kuhusu changamoto za wafugaji Ulega amesema, “Jambo hili limeshaelekezwa na linahusisha sekta mbalimbali, iko Tamisemi, mifugo na Ilani ya CCM imeelekeza wazi kuhakikisha ardhi inapimwa na kugawiwa kwa wafugaji, hili tutalifanyia kazi.”

Naibu Waziri wa Kilimo, Mary Mwanjelwa amesema anamshukuru Rais kwa imani kubwa aliyonayo kwake kwa kumteua.

“Nimepewa imani na Rais na lazima nithibitishe imani hiyo kwa kuiweka katika matendo, tegemeo la Watanzania ni kila mmoja aweze kufanikiwa,” amesema.

Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Stella Manyanya amesema atahakikisha Tanzania ya viwanda inafikiwa na kuifikisha nchi katika uchumi wa kati.

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza amesema, “Unapoaminiwa na Rais inapaswa kurejesha heshima hiyo. Nitafanya kazi kwa mujibu wa ilani yetu.”

Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Juma Aweso amesema, “Haijawahi kutokea Wilaya ya Pangani kuteuliwa mtu, anayelala na mgonjwa ndiye anayejua tatizo, tutaomba ushirikiano wa dhati kwa kila mmoja.”

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla amesema atatumia muda mwingi kuwekeza katika kutangaza vivutio vilivyopo nchini, akidai eneo hilo limekuwa na changamoto ikiwemo rasilimali fedha.

“Kuna changamoto ya jinsi tunavyotangaza vivutio vyetu na hili ni eneo ambalo nitawekeza nguvu zangu kutangaza vivutio,” amesema Dk Kigwangalla.

Amesema mgogoro wa Loliondo mkoani Arusha umekuwa ukizungumzwa kwa muda mrefu, hivyo atahakikisha unafikia mwisho

Mgogoro wa maeneo ya hifadhi hizi ni changamoto ambazo nazifahamu nitakwenda kuzifanyia kazi. Naibu Waziri wa Tamisemi anayeshughulikia watu wenye ulemavu, Stella Ikupa amesema, “Namshukuru mheshimiwa Rais kwa kuniamini ili kumsaidia kwa watu wenye ulemavu,  changamoto ni nyingi na tutahakikisha tunazishughulikia.”

Hafla ya kuapishwa mawaziri na manaibu hao imehudhuriwa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan; Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa; Spika wa Bunge, Job Ndugai; Jaji Mkuu, Profesa Ibrahim Juma; wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama na viongozi mbalimbali wa Serikali.

Rais Magufuli Waapisha Mawaziri Wapya, Awapa Mwongozo

Leave A Reply