The House of Favourite Newspapers

Mbasha Atangaza Mkesha Maalum Kumwombea Ruge

MUIMBAJI maarufu wa nyimbo za injili nchini, Emmanuel Mbasha, amesema mafanikio makubwa ya muziki nchini Tanzania yanahusiana kwa kiwango kikubwa na Mkurungezi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group, Ruge Mutahaba.
Mbasha ameyasema hayo kupitia ukurasa wake wa Instagram ambapo ameweka siku Ijumaa ya Novemba30,2018,  kwa ajili ya mkesha wa kumuombea Ruge ili aweze kupona.
“Ijumaa hii nitakuwa kwenye mkesha wa kufunga na kufungua mwezi, na katika mkesha huu nitakuwa na maombi maalum ya kumuombea Ruge Mutahaba ambaye yuko nchini Afrika Kusini kwa matibabu. Huyu ndugu binafsi tunafahamiana vizuri sana, maana alikuwa mtu wa karibu sana kwangu.
“Najua wengi hawajui kuwa Ruge ndiye aliyekuwa meneja wetu aliyeisimamia albam yetu ya kwanza na ya pili wakati tunaimba na mke wangu, na hata baadhi ya nyimbo zetu ni yeye alisimamia kwa umakini mkubwa nikishirikiana nae kwa ukaribu sana, na kuzisimamia hadi zikavuma kila kona na kujulikana.
“Na kupitia usimamizi huu wa Ruge tulisaini mikataba mingi sana iliyokuwa ya faida. Hata katika ndoa yangu Ruge alipenda kunitia moyo na kuniambia kuwa anafurahi kuona jinsi ninavyompenda mke wangu na kumsimamia vizuri, jambo ambalo ni gumu sana kufanywa na wanaume wengi wa Kiafrika. Kwa kweli katika mambo yanayohusu tasnia ya muziki Tanzania kwa ujumla Ruge ana mchango mkubwa sana kwenye hii sanaa.
“Si tu kwenye Bongo Fleva,  bali hata nyimbo za Injili maana hadi leo hii ukitazama wanamuziki wengi wa nyimbo za Injili ambao umaarufu wao umevuka ile mipaka ya kujulikana ndani ya kanisa tu, asilimia kubwa utakuta nyuma yao kuna support ya Ruge Mutahaba. Hivyo naamini hata katika ufalme wa Mungu huyu ni mtu wa faida sana. Na umuhimu wake umezidi kuonekana katika tukio la juzi la Fiesta, maana naamini kabisa endapo angekuwepo kila kitu kingeenda sawa.
“Nikiwa kama baba wa kiroho na mlezi mkuu wa waimbaji wote wa nyimbo za Injili Tanzania, napenda kutoa rai kwa wasanii wote Tanzania, huu ni wakati muafaka wa kila mmoja kuweka pembeni tofauti zake za u-team na tuungane kwa pamoja kumuombea dua njema ndugu yetu Ruge Mutahaba, na huu ndiyo moyo wa binadamu muungwana anayejua utu ni nini.
“Ila kwa yule atakayefurahia matatizo yake hakika atakuwa mchawi hata kama hajawahi kupaa na ungo. Maana ugonjwa ni hali inayompata mtu yeyote, leo kwake kesho kwako.
Asanteni….Get well soon brother Ruge,” amesema Mbasha.

Comments are closed.