The House of Favourite Newspapers

MBINU ZA KUMFUNGA BREKI MWANAUME ANAYESALITI PENZI

HOFU kubwa anayoweza kuwa nayo mwanamke aliye katika ndoa, au katika uhusiano wa kudumu, ni mumewe au mpenzi wake kumsaliti kwa kutoka na mwanamke mwingine! Wengi hubaki na hofu kubwa ndani ya mioyo yao kwamba itakuwaje kama mume au mpenzi atanogewa na utamu wa penzi la mchepuko?

 

Itakuwaje kama mume au mpenzi atasahau kila kitu kuhusu mambo yote waliyopanga pamoja? Ukizungumza na wanawake kumi ambao kweli wapo katika mapenzi ya dhati na wanaume wao, nane kati yao watakupa majibu kama hayo hapo juu. Wanaoishi na watu wasiowapenda ndiyo kundi pekee la wanawake ambao hawahofii kabisa waume zao kuchepuka.

 

Sasa kama wanawake wengi wanahofia kuwapoteza wanaume wanaowapenda, ni wangapi wanajua wanatakiwa kufanya nini ili ndoa ziendelee kudumu, mapenzi yaendelee kuwa matamu na uaminifu uzidi kudumu katika ndoa? Utashangaa kugundua kwamba wengi hawajui nini wanatakiwa kukifanya ili waendelee kujihakikishia nafasi kwenye ndoa au uhusiano waliopo, matokeo yake wanakuwa wanabahatisha tu.

 

Hujawahi kuona mwanamke anampenda sana mumewe lakini kila siku hawaishi kugombana? Zifuatazo ni mbinu zitakazokusaidia mwanamke kumroga mumeo kiasi kwamba hata anapoingiwa na ibilisi wa kutaka kukusaliti, mwenyewe arudishe mawazo nyuma na kuachana na alichokuwa anataka kukifanya.

 

KAULI NZURI Mwanasaikolojia mmoja nchini Uingereza, amewahi kueleza kwamba mwanamke anapokosa kauli nzuri ndani ya nyumba, akawa ni mtu wa kuongea hovyo, kufoka au kutukana, picha inayomjia mwanaume akilini mwake, ni mama mkali anavyomfokea mwanaye na wakati mwingine kumuadhibu.

 

Yaani ukiwa na kauli za hovyohovyo kwa mumeo, hatakuona kama mkewe, atakuona kama mama wa kambo mwenye roho mbaya ambaye kazi yako ni kumuwazia mabaya au kuunda njama za kumkomoa.

 

Kwa bahati mbaya, hakuna mtu anayependa kuonewa, kwa hiyo utaanza kuona mwanaume akiwa karibu na wewe, muda mwingi anajihami, hapendi mazungumzo ‘romantic’ na wewe na kama usipokuwa makini na ukawa unaendelea ‘kuchonga’, basi na yeye kama ana haiba ya ukali ataanza kukudunda, mwisho itakuwa ni kelele na ugomvi usio isha ndani ya nyumba.

 

Wana ume wanapenda lugha laini, zungumza naye kwa upole, mpe pole ya kazi anaporudi nyu mbani jioni, mkumbatie, mlalie kwenye kifua chake na kama mazingira yanaruhusu mbusu. Mshukuru anapokupa zawadi, mpongeze anapofanya vizuri na msifie anapostahili kusifiwa. Mnapokuwa peke yenu, jenga mazoea ya kuwa unamshika japo mkono wake, itawaleta karibu na unapokuwa na jambo lolote la kuzungumza naye, hakikisha unatafuta muda muafaka.

 

Utafiti unaonesha kwamba kauli nzuri peke yake, inaweza kumfanya mwanaume akamfanyia mwanamke hata jambo ambalo hakupanga kulifanya, anachotaka yeye ni wewe kufurahi.

 

UWAZI NA UAMINIFU Silaha nyingine kubwa inayoweza kumfanya mwanaume asifikirie kabisa kukusaliti na ajivunie kuwa na wewe, ni kuwa muwazi na mwanimifu kwake.

 

Unakuta mwanamke anahofia mumewe asimsaliti na kwenda kwa mwingine lakini yeye kutwa kuchati na wanaume hovyo kiasi kwamba hawezi hata kuiacha simu yake mumewe akaishika, akiiacha basi ameweka password kila sehemu.

 

Ukiwa na tabia ya aina hii, maana yake kuna mambo mengi unayomficha mwenzi wako na ndiyo maana huwezi kumpa simu yako akakaa nayo hata kwa dakika moja. Ukitaka mume akuheshimu, anza kwanza kujiheshimu wewe mwenyewe, acha mazoea yasiyofaa na watu wa jinsia nyingine. Itaendelea wiki ijayo.

Comments are closed.