The House of Favourite Newspapers

Mbosso Avunja Ukimya Vita Yake na Aslay!

0

STAA wa muziki wa Bongo Fleva na memba wa lebo kubwa ya muziki Bongo ya Wasafi Classic Baby (WCB), Mbwana Yusuf Kilungi ‘Mbosso Khan’, amevunja ukimya juu ya vita yake na msanii mwenzake, Aslay Isihaka.

 

Katika mahojiano maalum na Gazeti la IJUMAA WIKIENDA, Mbosso ambaye anatamba na wimbo wake wa Sina Nyota, anasema kuwa, yeye hana shida wala kinyongo na Aslay, kwa sababu haelewi ni nini kinaendelea.

 

“Mimi na wenzangu tuliokuwa wote Yamoto Band, tuko sawa japokuwa mawasiliano yetu ni hafi fu na kila mmoja ana uongozi wake.

 

“Kuhusu mimi kuwa na bifu na Aslay, naweza kusema sijui nini kilitokea kwa upande wake, maana mimi niko sawa. “Nakumbuka nilikuta amenifuta kwenye ukurasa wake wa Instagram (unfollow), nikashtuka sana na kujiuliza ni kwa nini imekuwa hivyo?

 

“Watu na kurasa za habari mitandaoni, wakaanza kuposti kitu hicho na sikuchukulia siriazi, nikaamua kuachana na hiyo ishu.

 

“Nikasema labda kuna mtu alimpa simu yake ndiyo akafanya hivyo au ni mtoto alichezea maana mimi ni mzazi, naelewa mambo hayo.

 

“Lakini kadiri siku zilivyokwenda, nikaona ni ishu ambayo iko siriazi, sikujua nini kinaendelea mpaka sasa na tangu siku hiyo wala sijataka kujitia ninauliza.

 

“Yeye (Aslay) ni binadamu na sikutaka kuingilia zaidi, maana ni uamuzi wake mwenyewe,” anasema Mbosso. Kuhusu kuzungumza pamoja, Mbosso anasema yeye hakai na kinyongo na hana tatizo.

 

“Mimi sina tatizo, watu wanatakiwa wajue sina tatizo na mtu.

“Sijui na wala siwezi kukaa na kinyongo ndani, maana mimi ni mwepesi wa kumwambia mtu neno samahani kuliko neno nakupenda.

 

“Mara nyingi neno samahani lina maana kubwa kuliko hata neno nakupenda na watu wajue hilo, sina tatizo kabisa,’’ anasema Mbosso ambaye yeye na Aslay wamepita kwenye mikono ya meneja wa wanamuziki Bongo, Said Fella ‘Mkubwa Fella’.

 

Alipotafutwa Aslay ili kusikia upande wake, meneja wake, Shaban Chambuso alisema kuwa, yupo visiwani Zanzibar, lakini akirejea Dar atawatafuta waandishi.

STORI: HAPPYNESS MASUNGA NA KHADIJA BAKARI, DAR

Leave A Reply