MBUNGE wa Singida Mashariki Tundu Lissu ambaye alipigwa risasi jana Alhamisi mjini Dodoma, anaendelea kupokea matibabu katika Hospitali ya Aga-Khan mjini Nairobi alikolazwa.
Kufikia saa 10 alasiri, madaktari walikuwa bado wanaendela na upasuaji wa zaidi ya saa 4 wakijaribu kutoa risasi zilizokuwa zimemdhuru kiongozi huyo wa upinzani.
Mwandishi wa BBC, Idris Situma amezungumza na mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ambaye aliongoza shughuli nzima ya kumkimbiza Lissu Nairobi, na alianza kwa kumuuliza hali halisi ya mgonjwa ikoje?
“Hali ya mgonjwa bado ni tete lakini madaktari wanatupa matumani atapona. Alipoteza damu nyingi sana kutokana na majeraha mengi ya risasi. Ameshafanyiwa upasuaji mpaka sasa amepumzika na anendelea na matibabu mengine ya kawaida,” alisema Mbowe.