The House of Favourite Newspapers

Mbunge Kibiti Sasa Avalia Njuga Kuing’arisha CCM Wilayani Humo

0
Mbunge wa Jimbo la Kibiti, Pwani, Mh. Twaha Mpembenwe.

 

 

MBUNGE wa Jimbo la Kibiti mkoani Pwani, Mh. Twaha Mpembenwe baada ya kusaidia shughuli mbalimbali za kijamii kwa kujenga majengo mapya kwenye hospitali, shule na kutoa misaada mbalimbali katika jimbo hilo sasa ameamua kuzing’arisha ofisi za CCM jimboni humo ambapo juzi Jumamosi viongozi na wanachama wa CCM jimboni humo wamepokea vifaa vya ujenzi kwa ajili ya ukarabati wa jengo la ofisi ya wilaya hiyo ambavyo vilitolewa na wahisani wanaomuunga mkono mbunge huyo kwa jitihada zake za kimaendeleo ambaye sasa amegeukia kwenye kuzing’arisha ofisi cha chama hicho.

Matofari yakiendelea kufyatuliwa.

 

 

Miongoni mwa vifaa vilivyopokelewa kwenye hafla hiyo ni pamoja na gypsum board na vinginevyo ambavyo ni kwaajili ya kumalizia ofisi hiyo.

Vifaa hivyo vimetolewa na wadau wa maendeleo jimboni humo, Chama cha Ushirika mkoa wa Pwani (CORECU) chini ya Mwenyekiti wake, Mussa Mng’aresa katika kuunga mkono juhudi za Mbunge Mpembenwe ambaye sasa ameamua kuzivalia njuga ofisi za CCM jimboni na kutaka ziwe za kisasa.

Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika mkoa wa Pwani, CORECU Mussa Mng’eresa (kulia) akimkabidhi sehemu ya gypsum mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kibiti, Pwani Abdul Jabir Marombwa kwa niaba ya Mbunge Mh. Mpembenwe ambaye hakuwepo kwenye hafla hiyo.

 

 

Pamoja na CORECU naye mfanyabiashara wa Cosmas Sisa anayefanyia shughuli zake, Kibiti Barabara ya Kilwa amechangia vifaa kadhaa vya ujenzi katika kumuunga mkono juhudi za Mbunge Mpembenwe.

 

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Katibu wa CCM Wilaya ya Kibiti, Muhidini Zakaria amesema;

Katibu wa CCM Wilayani Kibiti, Muhidini Zakaria akizungumza na wanahabari baada ya kupokea mchango huo kutoka kwa wadau wanaounga mkono juhudi za mbunge Mh. Mpembenwe.

 

 

”Leo tumekusanyika hapa kwa ajili ya kupokea vifaa vya ujenzi ikiwemo gypsum board na vinginevyo kwa ajili yakumalizia ofisi ya CCM wilaya ya Kibiti.

 

“Hizo zote ni jitihada za Mbunge wa Kibiti, Mh. Twaha Mpembenwe ambaye sasa ameamua kuwekeza nguvu kwa chama cha Mapinduzi kuanzia ngazi ya matawi kata na wilaya.

Mafundi wakiendelea na ujenzi.

 

 

“Alianzia kutoa misaada ya kjamii kwenye ngazi ya kata kisha wilaya ambapo kata ya Mlanzi, Mtawanya, Mjawa na kwingineko ametoa mifuko mingi ya saruji na mabati nondo na vifaa vingine vya ujenzi kwa ajili ya majengo ya serikali na hata kuwasaidia wananchi waliokumbwa na kimbunga walipoezuliwa mapaa na kubolewa nyumba zao na kimbunga miezi michache iliyopita.

“Mbunge Mh. Mpembenwe sasa amekuja na kipaumbele cha kuyang’arisha majengo  akianza na jengo CCM Wilaya ya Kibiti kwa kuliwekea bati mpya tiles, madirisha ya vioo , fisherboard na kulifanya kuwa la kisasa zaidi.

Mfanyabiashara Cosmas Sisa akielezea jinsi alivyovutiwa na kasi ya Mbunge Mpembenwe na kuamua kumuunga mkono katika juhudi zake za kukijenga chama.

 

 

“Lengo la Mh. Mpembenwe ni kutaka kuhakikisha hadi kuelekea uchaguzi mkuu wa ndani wa CCM ngazi ya Wilaya mwezi September 21 tuwe tumemaliza jengo letu hili la CCM Wilaya na liwe na ukumbi mkubwa ambalo tutalitumia kwa ajili ya vikao vya chama na miradi mbalimbali ya CCM Wilaya.

Kazi ikiendelea.

 

“Katika kumalizia jengo hili, Mh Mpembenwe ametoa mifuko 600 ya saruji ambayo itasaidia kufyatua matofali 15,000 yatakayotumika kujenga ukumbi na uzio kwenye jengo hilo”. Alimaliza kusema Katibu huyo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika Mkoa wa Pwani, CORECU, Mussa Mng’eresa amesema ofisi yake  imeamua kutoa msaada huo wa gypsum ikiwa ni jitihada zao za kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan katika utekelezaji wa ilani ya  CCM na Mbunge wa Jimbo la Kibiti, Mh Twaha Mpembenwe.

HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS NA ISSA MNALLY/ PWANI

Leave A Reply