ALIYEKUWA mbunge wa jimbo la Dimani Zanzibar, Abdallah Sharia Amer na Athumani Rajabu leo Julai 11, 2018 wamepandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za utapeli.
Mwendesha mashtaka wa serikali, Janet Magoho, akiwasomea hati ya mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi. Hamisi Ally. amedai kuwa washtakiwa walitenda kosa hilo la kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu kati ya Julai 17 na Septemba 29 mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Imedaiwa siku hiyo washtakiwa hao kwa pamoja na kwa kudanganya, walijipatia kutoka kwa Dkt. Abdi Hirsi Warsame kiasi cha milioni 55 kwa kumdanganya kuwa wangemsambazia vifaa tiba vya hospitali huku wakijua kuwa siyo kweli.
Hata hivyo, washtakiwa wote wamekana kutenda kosa hilo na wamerudishwa rumande kwa kushindwa kutimiza masharti ya dhamana ambapo wametakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya shilingi. Mil. 27.5 kila mmoja.
Pia wametakiwa kuwasilisha fedha taslimu kiasi cha Sh. 27.5 au kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya kiasi hicho cha fedha.
Kwa mujibu wa upande wa mashtaka, upelelezi katika kesi hiyo bado haujakamilika na kesi hiyo imeahirishwa hadi kesho Julai 12 mwaka huu kwa ajili ya dhamana.
Comments are closed.