MANCHESTER City ni kama wameongezewa nguvu katika mbio zao za kumshawishi Lionel Messi kuhamia kwenye timu yao hiyo, hatua hiyo inakuja baada ya staa huyo kutoa kauli kuwa amechoka kulaumiwa kila mara ndani ya Barcelona.
Messi, 33, alifuatwa na watu wa kodi wa Hispania mara baada ya kurejea nchini humo akitokea kwenye majukumu ya timu ya taifa ya Argentina ambapo walishinda mabao 2-0 dhidi ya Peru.
Amesema kuwa amechoka kuwa tatizo ndani ya Barcelona, kauli ambayo inaendeleza mwendelezo kuwa hana furaha ndani ya timu hiyo akiwa amesaliwa na miezi kadhaa kabla ya kumaliza mkataba wake. Kauli hiyo ilikuja baada ya kudaiwa kuwa amekuwa sehemu ya tatizo kwa mshambuliaji mwenzake, Antoine Griezmann kutofanya vizuri, kauli ambayo ilitolewa na wakala wa zamani wa Griezmann, Eric Olhats.
Kuhusu suala la wasimamizi wa kodi, Messi alisema: “Nimefika tu na ninakutana na maswali ya watu wa kodi, inashangaza na inaumiza.” Messi na baba yake ambaye ni wakala wake pia, Jorge alikutwa na hatia kuhusu masuala ya kodi mwaka 2016 na wakatakiwa kutumikia kifungo cha miezi 21 jela, lakini haikuwa hivyo baada ya kulipa faini ya pauni 1.5m.
Matukio kama hayo yanaongeza presha ya Messi kuwa yupo njiani kuondoka Hispania hasa kwa kuwa Man City imekuwa ikimuwania kwa ukaribu. City haijakata tamaa kuhusu kumsajili Messi ambapo imekuwa ikimtumia kocha Pep Guardiola kama sehemu ya ushawishi kutokana na urafiki wake na Messi.
Barca imekumbwa na mtikisiko wa kiuchumi tangu kuibuka kwa maambukizi ya Virusi cvya Corona na imekuwa na wakati mgumu katika masuala ya fedha, ikishindwa kukamilisha mpango wa kumsajili mshambuliaji wa Lyon, Memphis Depay katika dirisha la usajili lililopita.
BARCELONA, Hispania