Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega amesema Serikali ya Viwanda inakwenda na ufugaji, zikiwemo miradi ya kuku na samaki kwa ikiwa ni moja ya njia ya kuinua uchumi na pato kwa Watanzania na taifa kwa ujumla.
Ulega aliyasema nayo wakati wa ziara yake aliyoifanya Wilaya ya Mkuranga-Pwani kwenye vijiji Vinne ,ambapo alisema hakuna sababu ya wananchi wa Mkuranga kuchukua Kuku mikoa mingine wakati wanaweza kufuga wenyewe na kujipatia kipato na maendeleo sanjari na kuuza kwa mikoa mingine.
Katika kuonesha utayari wa kufanikisha hilo, Ulega ambaye pia ni Mbunge wa Mkuranga na kada maarufu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), alisema yuko tayari kusaidia kwa kujitolea kutafuta na kuajiri maafisa na wabobezi wa masuala ya ufugaji hususan kuku na samaki ili waweze kutoa elimu stahiki kwa wakazi wenye nia na lengo la kufuga.
“Soko la kuku na samaki ni kubwa sana kutokana na ukweli kwamba vitoweo hivyo ndivyo vyenye kuhitajika kwa wingi kwa hiyo kuna kila sababu ya kujikita kwenye ufugaji, lakini lazima tuwe na elimu tosha juu ya ufugaji hususani kuku na samaki, ndugu zangu tunaposema Tanzania ya Viwanda ni pamoja na ufugaji.
“Inawezekanaje wakazi wa Mkuranga kuagiza kuku kutoka Singida kwa mfano, wakati tunao uwezo mkubwa wa kufuga? Binafsi niko tayari kama mbunge na waziri kujitolea kikamilifu kuhakikisha zoezi hili linafanikiwa ambapo nitaajiri wataalamu wa mifugo ndipo hatua zingine zifanyike, lazima tudhamirie kuibadili nchi yetu kwa kuinua uchumi kwa kujikita kwenye viwanda na hii ni kwa nchi nzima,” alisema Ulega.
Katika ziara yake hiyo ya siku mbili kikazi kwa jimbo la Mkuranga na viunga vyake, Ulega aliaahidi kuchagia
Sh. Milioni Moja na mifuko ya saruji kwa ajili ya kikundi cha VICCOBA cha wanawake waliojenga ukumbi wa mikutano na sherehe kilichopo Mwandege.
NA DENIS MTIMA/GPL