The House of Favourite Newspapers

‘Mfalme Zumaridi’, Wenzake Wafikishwa Mahakamani, Waomba Dhamana

0

Diana Bundala maarufu kama ‘Mfalme Zumaridi’ na wenzake 83 leo wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mwanza kwa ajili ya kusomewa maelezo ya awali ya mashtaka yanayowakabili.

 

Zumaridi na wenzake wanakabiliwa na makosa matatu ikiwamo ya usafirishaji haramu wa binadamu, shambulio la kudhuru mwili na kuzuia maofisa wa Serikali kutimiza wajibu wao.

 

Wakati wa kuwasili ndani ya chumba cha mahakama Zumaridi ameonekana akiwa amejifunika na kitenge wakati wote kisha akalazimika kukiondoa baada ya kupanda kizimbani kusomewa maelezo hayo.

 

Hata hivyo, washtakiwa hao hawakusomewa maelezo ya awali ya mashtaka yanayowakabili kutokana na Hakimu Mkazi mwandamizi, Monica Ndyekobora ambaye ndiyo mwenye mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo kutokuwepo leo mahakamani jambo lililosababisha mashauri hayo kusikilizwa na Hakimu Mkazi mkoa wa Mwanza, Stela Kiama.

 

Washtakiwa baada ya kufikishwa mahakamani wamesomewa mashtaka yanayowakabili na wakili wa Serikali Mwandamizi anayeendesha mashtaka hayo, Emmanuel Luvinga akishirikina na Gisela Bantulaki.

 

Katika shauri hilo, kuna mashtaka matatu yanayowakabili washtakiwa hao ambayo ni kesi ya jinai namba 11/2022 ambayo ni usafirishaji haramu wa binadamu inayomkabili mfalme Zumaridi peke yake, kesi ya jinai namba 10/2022 ambayo ni kufanya shambulio la kudhuru mwili kwa lengo la kuzuia maofisa wa serikali kutimiza wajibu wao linalomkabili Zumaridi na wenzake 8.

 

Nyingine ni kesi ya jinai namba 12/2022 inayomkabili mhubiri huyo na wenzake 83 ambayo ni kufanya kusanyiko lisilo rasmi.

 

Baada ya Washtakiwa kusomewa mashtaka hayo, wakili wa utetezi, Erick Mutta aliwasilisha maombi ya dhamana kwa washtakiwa wanane wanaoendelea kusota rumande na mhubiri huyo ambayo yalikubaliwa na mahakama hiyo baada ya washtakiwa kukidhiri vigezo na masharti ya dhamana.

 

Kwa upande wake, Mfalme Zumaridi kutokana na kukabiliwa na kesi ya usafirishaji haramu wa binadamu isiyo na dhamana anaendelea kusota rumande na washtakiwa wenzake nane ambao hawajakidhi vigezo vya kupewa dhamana.

 

Shauri hilo limeahirishwa hadi Aprili 4 mwaka huu litakapoitwa kwa ajili ya kusomwa maelezo ya awali kwa washtakiwa.

 

Katika hatua nyingine, wakili wa utetezi Erick Mutta ameiambia mahakama hiyo kwamba, mshtakiwa namba 67 (Elias Joseph) ameshindwa kufika mahakamani hapo kutokana na maofisa kutoka Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) kufika ofisi kwake kwa ajili ya kumfanyia ukaguzi.

 

Amesema mshtakiwa namba 38 (Maria Joseph) ameshindwa kufika mahakamani hapo kutokana na kulazwa katika hospitali ya rufaa ya Kanda ya Bugando akipatiwa matibabu ya majeraha aliyopata wakati wa ukatamaji uliofanywa na maofisa wa Jeshi la Polisi mkoani humo.

 

Pia amesema mshtakiwa namba 84 (Kanyangi Mary) na 68 wameshindwa kuhudhuria shauri hilo kutokana na kuhudhuria matibabu katika hospitali.

Leave A Reply