The House of Favourite Newspapers

MGOMBA HAUZAI EMBE

PAMBEEEE shoga wanakwambia ukimuona ngedere mjini basi ujue ana mwenyewe ati! Wareee reeeeee! Maskini hana mpambe na mjini hulali njaa ila utachelewa kula, upo nyonyo? 

 

Shoga kichaa hajipeleki hospitali, nashanga umekuja mjini unajua kukunja ngata umejua kuvaa dera unatusumbua, inahu! Hakuna kitu kinanikera shoga yangu kama mtu kujifanya anajua kumbe hajui, utabaki kuwa jogoo tu asubuhi kuwika kufungua mlango huwezi, heee heeeiyaaaa!

 

Usinione leo nimekuja na michambo basi ukajua Anti Naa nina furaha, hakuna kitu kinanikera kama kumuonea mwanamke halafu baadaye unakuja unajifanya unajuta, shuuutuuu! Siku zote nikisema namaanisha shoga na leo nipo na nyie wanaume mnaojiita wanaume kumbe wanaume suruali, wanaume mdomoni lakini kuyaishi maisha mnaigiza!

 

Hii imekuja baada ya juzi kupokea meseji kwa shosti wangu mmoja ambaye nilisoma naye miaka ya nyuma, alishangaa kunikuta nawapa vichambo kwenye gazeti kwa sababu sikuwa mtu wa aina hiyo, haaloooooo ehhhhh nicheke miye mbavu zangu zitanuke!

 

Basi huyo shosti wangu anasema kuwa, alikuwa na mwanaume wake wa kwanza ambaye yeye binafsi alimpenda sana kumbe yule mwanaume wala hakuwa na nia naye, akapewa mimba na baada ya kujifungua yule mwanaume akaenda kuoa mwanamke mwingine na kumuacha kwenye mataa.

 

Baada ya kukaa miaka minne akilea mtoto wake akapata bahati ya kukutana na mwanaume mwingine ambaye alimpenda lakini hakutaka kumuoa kisa amezaa na mwanaume mwingine, basi unaambiwa yupo tu anajiona kama mtu aliyekosa bahati ya maisha.

Shoga kuna vitu vinatia hasira kama siyo uchungu, hivi wakati mwingine tuseme tu hivi nyie wanaume wa aina hii nani aliyewaumba, kwa nini umzalishe mwanamke wa watu halafu ukatae kumuoa? Haya sasa akipata mwanaume anayejua kulea akaamua kumchukua na mtoto akamsomesha utasema huyo ni mtoto wako? Sura lako utalificha wapi mtoto huyo kesho na keshokuta anakuja kuwa kiongozi mkubwa nchini? Shuuuutuuuu!

 

Shoga mgomba hauzai embe hata siku moja, usipotambua kuwa mwanamke aliyezalishwa naye ana haki ya kuolewa utakuwa upo dunia ya mbali sana. Sitaki kusema sana ati, tukutane tena wiki ijayo kwa mada nyingine kali zaidi ya hii. Ni mimi Anti Naa Shangingi Mstaafu!

Comments are closed.