Miujiza Ndoa ya Mondi na Zuchu
LICHA ya mwenyewe kutoanika kinaga ubaga kuhusu mkewe mtarajiwa, lakini kuna mambo yameanikwa ambayo yanashangaza endapo staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ ataamua kuingia kwenye ndoa na mtoto mzuri Zuhura Othuman ‘Zuchu’, IJUMAA WIKIENDA linakupa habari mpya inayowahusu!
MNAJIMU AFUNGUKA
Hiyo imetokana na gazeti hili kuzungumza na Mnajimu Maalim Hassan Yahya Hussein, ambaye pamoja na mambo mengine, ameeleza maajabu ya nyota za wawili hao na jinsi ambavyo zinashabihiana na kwamba, watafanya makubwa wakiwa pamoja.
“Zuchu na Mondi nyota zao zinaendana, kwa sababu ni mizani na ng’e, maana ni nyota ambazo ziko jirani, kama wataamua kuwa pamoja na kuoana, watakaa vizuri.
“Katika mwezi wa kumi mwishoni, inaanza nyota ya ng’e, hivyo Diamond kazaliwa Oktoba nyota yake ni mizani na Zuchu kazaliwa Novemba nyota yake ni ng’e, ndivyo nyota zao zinavyoonesha jinsi gani zilivyo karibu.
ATAJA ASILI…
“Mwenye nyota ya ng’e asili yake ni maji na nyota ya mizani asili yake ni hewa, ukiangalia kemistri hapo, maji yanatengenezwa na hewa, hivyo kati yao mmoja anamtengeneza mwingine (Mondi anamtengeneza Zuchu).
“Kile wanachokifanya Zuchu na Diamond, ndicho kinachotakiwa kuwa kama sayansi inavyoonyesha, hiyo ni sawa sawa kabisa hata katika masuala ya kimuziki, ni sawa jinsi Diamond anavyomshika mkono Zuchu kwa sababu ni muingiliano na kuendana kwa nyota zao,’’ alisema Maalim.
DIAMOND KUCHELEWA KUOA
Mbali na kutabiri juu ya ndoa ya Mondi na Zuchu, Maalim aliongeza kwa kusema kuwa, nyota ya Mondi asili yao wana kawaida ya kuchelewa kuoa.
“Watu wenye nyota ya mizani huchelewa kuoa na akiamua kuoa, anaangalia nini atapata kama ni faida ama hasara. “Sababu hiyo huwafanya kuchukua muda mrefu na anakuwa si yeye, bali ni nyota yake inamsukuma kufanya hivyo.
“Kama Diamond kasema anataka kuoa mwaka huu, basi na itakuwa hivyo, kinyota ndivyo inavyoonyesha, pia nyota zao ni za mapenzi na wanapendwa mno,’’ alimalizia kwa kusema Maalim Hassan.
Katika moja ya kauli ambazo Mondi aliwahi kuzungumza kwenye vyombo vya habari ni kuwa, Oktoba 2 mwaka huu ambayo ni siku yake ya kuzaliwa ataoa, lakini hakutaja mhusika atakayefunga naye ndoa hiyo.
STORI: HAPPYNESS MASUNGA NA KHADIJA BAKARI