IKIWA imepita miezi kadhaa tangu dada wa mwanamuziki wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Mwanahawa Abdul ‘Queen Darleen’ aolewe na mfanyabiashara Isihaka Mtoro, tayari chokochoko zimeanza.
Habari mpya zilidai kuwa, mke mkubwa wa jamaa huyo aitwaye Sabra, amekuwa akiirushia ndoa ya Darleen ambaye ni first lady wa Lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB).
Hivi karibuni mke huyo mkubwa alidaiwa kusambaza video zake kadhaa mitandaoni akiimba nyimbo za Taarab zilizosheheni vijembe.
“Hivi mnajua kama Isihaka anampenda sana yule mke wake mkubwa?
“Huwezi kuamini, siku ambayo Isihaka alikwenda kumuoa Darleen, hakumpa taarifa mkewe. Sasa kutokana na taratibu za dini, mwanaume akioa bila kumtaarifu mkewe, inabidi ampe zawadi ya kitu chochote. Kwa hiyo, ili kuweka mambo sawa, ikabidi Isihaka amnunulie mke mkubwa gari na kumpa pesa taslim.
“Pia yule dada (mke mkubwa) amejengewa bonge la mjengo Kimara (Dar) na hati za nyumba zimeandikwa kwa jina lake.
“Huyo Darleen yeye amepangiwa tu nyumba.
“Ndiyo maana mnaona Isihaka hawezi kumuongelea vibaya mke wake mkubwa kwa sababu anamheshimu na kumpenda sana,” kilimwaga ubuyu chanzo ambacho ni mtu wa karibu na familia hizo.
Baada ya kupewa mchapo huo, Gazeti la IJUMAA WIKIENDA lilimtafuta mwanamke huyo mkubwa ambapo alikuwa mkali na kutoa povu kwamba, hana shida ya kuzungumza na waandishi badala yake atafutwe huyo mke mdogo (Darleen) maana yeye ndiye limbukeni wa ndoa.
“Mimi sina shida na wala sihitaji kuzungumza na waandishi wa habari, mtafuteni huyohuyo bi mdogo (Darleen) ndiye aongee kwa sababu yeye ndiye limbukeni wa ndoa; kutwa anamposti mume wangu kwenye akaunti yake.
“Mimi sina muda huo wa kuanza kuongea,” alisema Sabra na kukata simu.
Gazeti hili pia lilimtafuta Darleen ili azungumzie ishu hiyo ambapo alifunguka;
“Unajua mimi sijamsikia akiongea, hivyo siwezi kuongea chochote na kuhusu yeye kujengewa nyumba nzuri na mimi kupangishiwa, pia ninajisikia kawaida tu kwa sababu mwisho wa siku huwezi kuzuia watu kuongea.
“Niwaombe tu wananzengo, nao wapambane na uhusiano wao kwa sababu kila mtu ana uhusiano wake na anajua jinsi ya kudili nao na kuupa thamani, hivyo watulie, waache kuongelea ndoa za watu,” alisema Darleen.
STORI: RICHARD BUKOS, DAR