The House of Favourite Newspapers

Mkemi: Simba Wakiwahonga Mbeya City Watufunge Poa Tu

0
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Salum Mkemi (wa pili kutoka kulia) akiwa na watangazaji wa Kipindi cha Spoti Hausi  Saleh Ally (kulia), Philip Nkini (wa tatu kutoka kulia) na Wilbert Molanda (kushoto).

Mwandishi Wetu, | CHAMPIONI| Dar es Salaam

WAKATI Ligi Kuu Bara ikielekea ukingoni, Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Salum Mkemi, amefanya mahojiano maalum na Kipindi cha Spoti Hausi, kinachorushwa hewani na Global TV Online. Mahojiano hayo yalifanyika juzi Alhamisi.

Vipi kuhusu mbio za ubingwa?

“Presha ni kubwa ukiangalia kiukweli takribani miaka minne kipindi kama hiki tulikuwa tunakimbizana na Azam ambapo katika miaka hiyo, sisi tumechukua mara tatu na Azam mara moja.

“Lakini safari hii wamekuja Simba, ukiiangalia ni timu kubwa na huwezi kuifananisha na Azam kwa sababu wana wachezaji wengi wenye uzoefu na wana uchu wa miaka minne kutochukua ubingwa na huu unakwenda mwaka wa tano.

“Niwaambie tu siku zote mlima utakuwa mlima na kichuguu kitabaki kuwa kichuguu.”

Hebu fafanua hapo mwisho

“Yanga ni timu kubwa kuliko Simba, Yanga imeanzishwa mwaka 1935 na Simba 1936, sisi ni kaka zao, hivyo tunakwenda kuweka historia kwa kuchukua ubingwa mara ya 28 na ya tatu mfululizo, japo hili ni gumu lakini tunakwenda kulifanya kweli.”

Kuna sakata hili la straika wenu, Donald Ngoma kutimka, tuweke wazi alikwenda wapi na alikwenda kufanya nini?

“Ngoma alikwenda Afrika Kusini na amerudi. Alikwenda kufanyiwa matibabu kwa sababu tuliona hospitali nyingi za hapa nyumbani amekuwa akienda na kurudi, lakini akicheza mechi kidogo anaumia palepale, ukiangalia kwa sasa tunatakiwa ile kiweledi kuachana na kutegemea zaidi hospitali hizi za ‘local’ ambazo nyingi hazina uhakika, hivyo ni vizuri zaidi kwenda nje kujiangalia zaidi.”

Kwa hiyo tutarajie kumuona kwenye mechi hizi zilizosalia?

“Sidhani, kwa sababu ndiyo kwanza amerudi, lakini itategemea na mwalimu amemuona vipi.”

Kwa mwendo mnaokwenda nao Yanga hivi sasa, unadhani kuna kizuizi ndani yenu kinaweza kuwazuia kuchukua ubingwa?

“Kwa ndani hatuna shida yoyote kuanzia wachezaji mpaka viongozi, ugumu unakuja uwanjani kwa sababu mnapocheza kuna timu nazo zinahitaji pointi, ukiangalia Mbeya City wapo kwenye hatari ya kushuka daraja, Toto nao wapo kwenye hatari hiyo halikadhalika Mbao.

“Hizo timu haziwezi kukubali kushuka daraja kizembe na zaidi ni kwamba Mbao walitufunga kwenye Kombe la FA na kututoa, kwa hiyo hatutakuwa na mapambano rahisi ndiyo maana nasema ugumu upo kwa sababu hatuendi kushindana na miti, tunaenda kushindana na watu.

Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga, Salum Mkemi (kushoto) akipiga picha na Kocha Mkuu, George Lwandamina (katikati).

Kwa nini msijiendeshe wenyewe ilihali mna vyanzo vya kujiendesha na si kurudi kuomba msaada kwa wanachama?

“Tulikuwa tumekaa kama viongozi kulijadili hilo, lakini tukawasikia mashabiki na wanachama wakisema kama Yanga haina mdhamini na hamna pesa basi tuwape namba wachangie, tukawapa.

“Unajua lazima uende na akili za watu wanavyotaka, tukawapa namba wachangie, matokeo yake walianza watu 3,000, wakaja 200, na mpaka jana (Jumatano) walichangia watu 16, kwa hiyo wao wenyewe wameonekana kuisusa klabu yao mapema.

Mpaka sasa wamechanga kiasi gani?

“Kuna kama milioni kumi ambazo hizo ni kutoka kwa wanachama wetu nchi nzima na wamechanga kama wiki mbili hivi.

“Unajua ni rahisi kusema kitu kuliko kutenda, hata mimi nilivyokuwa nje ya uongozi nilisema viongozi wanashindwa kuiongoza timu, wangeweza kuwachangisha wanachama shilingi 50 na ukapata hela nyingi, kumbe watu wakikaa wanachokiongea ni tofauti na kutenda.

“Timu kama Yanga ni lazima uwe na mtaji mkubwa wa udhamini na si kutegemea mtu mmoja kuiendesha, mwanachama kuchangia ili aiendeshe Yanga haiwezekani, sisi tulitaka kuwaonyesha kwamba wanachokisema si sahihi na kweli majibu tumeyapata.”

Kifedha, unafaidika na nini ndani ya Yanga?

“Kifedha napata sifuri kwa sababu natoa fedha zangu naongezea pale panapokwama huku nikiwa sipati kitu, ndani ya Yanga hakuna mianya ya kujipatia pesa hovyo.

“Ukiangalia ndani ya Yanga mishahara ya mwezi kwa wachezaji na wafanyakazi wote inaweza kufika milioni 120, sasa hata ukicheza mechi tano kwa mwezi hupati hata shilingi milioni 50.

“Tumecheza na Kagera tumepata shilingi milioni 1.5 na maandalizi ya mechi inaweza kufika shilingi milioni 10.

Kwa hiyo upo kwenye biashara ya hasara?

“Hapana bali nipo kwenye uongozi na sifanyi biashara, ile ni dhamana na tumepewa kama dhamana ya uongozi kwa sababu wewe mwanao ili ale ni lazima ufanye njia yoyote, ukaibe, unyang’anye ilimradi mtoto ale tu.

Kwa hiyo ndiyo maana wachezaji wanagoma kwa kukosa hela?

“Ndiyo, lakini wakigoma ni lazima tutafute namna ya kuwapatia haki yao, sisi waajiri na soka ni ajira yao, wana familia wale, na wanapokosa kitu wanachotakiwa  kukipata ni lazima agome.”

Katika usajili, tuambie mustakabali wa wachezaji wanaomaliza mikataba upoje?

“Tuna wachezaji wengi mwisho wa msimu, mikataba inamalizika na tuliwaambia tunataka mikataba tuifanyie ‘review’ na kama kuna mchezaji ataona hawezi kuendelea kuwa Yanga, alete barua sisi tutamruhusu.

“Tunataka kuwa na wachezaji watakaoipigania timu, tunataka kuwa na wachezaji wanaoweza kuwa kwenye shida na raha.”

Ligi inapokuwa inakwenda ukingoni, kuna hizi ishu za kununua mechi, mara ngapi wewe umehonga?

“Sijawahi kufanya hivyo, mfano sisi tunacheza na Mbeya City, Simba wakitoa pesa kuwapelekea Mbeya City ili watufunge sisi haina shida kwa sababu naiona kama ni kuwapa hamasa, lakini wakileta kwa wachezaji wetu ili tufungwe ndiyo shida, wakipeleka kwa mwamuzi ni shida.”

 

Mashabiki na wanachama wa Yanga wanaamini mnakuwa na bajeti ya kamati ya ufundi ya kwenda kwa waganga, ni kweli?

“Kamati ya ufundi ni kocha na wenzake, ni uwendawazimu kutumia mamilioni ya pesa kwa kufanya usajili wa wachezaji na kocha, halafu unakuja kusaka waganga wakusaidie.”

Leave A Reply