The House of Favourite Newspapers

Mkongo Yanga Awapa Wachezaji Mbinu Mpya

Kikosi cha timu ya Yanga.

KOCHA mpya wa Yanga, Mkongomani Zahera Mwinyi, ametuliza mizuka ya wachezaji kwa kuwataka wacheze mpira mwingi na wala wasiichukulie mechi ya leo kama kitu cha ajabu sana mpaka kufikia hatua ya kupaniki. Mwinyi ambaye anazungumza kiswahili chenye lafudhi ya Congo, amewaambia wachezaji kwamba suluhisho la kuifunga Simba ni kutawala mchezo kwa kuuchezea mpira mara nyingi kadri inavyowezekana.

 

Kocha huyo alitoa maelekezo hayo kwa wachezaji kambini, na kuwasisitiza kwamba wasihofie ujio wake kwa vile hatabadilisha mambo mengi lakini atawaongezea uwezo zaidi kwa vile wote wako vizuri.

 

“Kocha anaonekana yuko fiti sana na kama tutapata muda mzuri wa kuwa naye naamini tutatisha sana huko mbeleni, huwezi kuamini baada ya kuanza kutufundisha alituambia tucheze sana mpira kwani njia pekee ya ushindi ni kujituma kwa kucheza kwani ukiweza kumiliki mpira muda mrefu utakuwa na uhakika wa kupata matokeo mazuri kwa mpinzani wako yeyote,” alidokeza mchezaji mmoja nyota wa Yanga.

Kocha mpya wa Yanga, Mkongomani Zahera Mwinyi.

“Anaonekana ni mtu wa fiziki sana ingawa ameanza kwa kututaka tucheze mpira mwingi muda wote, kingine ambacho nimekiona kwake ana tofauti sana na George Lwandamina kwani yule alipenda mpira wa taratibu ila huyu yeye anataka kasi na wenye pasi nyingi.

 

 

“Ametukataza tusimhofie kwa lolote zaidi tucheze kama tumekuwa nae siku zote kwani hapendi kututia hofu wala kutufanya tumuone kama mpya na ndiyo maana katutaka hata mechi yetu na Simba tuichukulie kawaida tu kwani kufanya hivyo kutatufanya tucheze bila kuwazia kelele za mashabiki,”aliongeza mchezaji huyo.

 

 

“Katuhakikishia ushindi ni mkubwa tu kwa wapinzani wetu kwani anawafahamu vizuri ingawa hajawahi kucheza nao akiwa kocha wa klabu, huwezi kuamini kama maneno yake pekee yametuliza mzuka wa kuiwazia Simba na ukianglia kwa sasa hapa kambini kwetu hakuna mchezaji mwenye hofu.”

 

Kocha huyo hatakuwa kwenye benchi leo kutokana na taratibu za kibali chake cha kazi kuchelewa huku akiwa pia amekaa muda mfupi na wachezaji, hivyo Noel Mwandila na Shadrack Nsajigwa ndiyo watakaobeba dhamana.

STORI NA MUSA MATEJA, SPOTI XTRA

Comments are closed.