The House of Favourite Newspapers

Mkuu wa BBG Amtaka Nkurunziza Kurejesha Matangazo ya VOA

Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Marekani ya kuratibu matangazo ya Mashirika ya Serikali (BBG) ambayo inasimamia VOA, John F Lansing.

 

Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa Bodi ya Usimamizi wa Utangazaji wa Mashirika ya Serikali ya Marekani – BBG –  ambayo inasimamia Shirika la Habari la Sauti ya Amerika (VOA), John Lansing, jana Jumatatu alitoa wito kwa Rais wa Burundi, Pierre Nkurunziza, kubatilisha uamuzi wa serikali yake wa kupiga marufuku matangazo ya VOA nchini humo, kama njia ya kuimarisha usalama, kuzuia ghasia na kulinda raia wa Burundi.

 

Katika taarifa iliyotolewa, Lansing alisema kuwa bodi hiyo itaendelea kuwaunga mkono raia wa Burundi kwa kutoa matangazo ya kuaminika na yasiyopotosha. Taarifa hiyo ilifuatia hatua ya serikali ya Burundi ya kusitisha matangazo ya VOA kwa muda wa miezi sita nchini humo kuanzia jana Jumatatu.

 

Hatua hiyo ilijiri siku moja baada ya dunia kuadhimisha siku ya Uhuru wa uandishi wa habari, na siku kumi tu kabla ya kura ya maoni nchini Burundi ambayo huenda ikabadilisha ukomo wa mihula ya urais. Waandishi wa VOA nchini Burundi walithibitisha kwamba sitisho hilo lilianza kutekelezwa kama serikali ilivyokuwa imesema.

 

“Ingawa VOA pia hutangaza katika mawimbi ya masafa mafupi, televisheni na kupitia mtandao katika nchi hiyo, hapana shaka kwamba matangazo ya redio kupitia masafa ya FM ndiyo maarufu zaidi nchini Burundi,” alisema Lansing.

 

Aliongeza kuwa raia wa Burundi wamekuwa wakitegemea Sauti ya Amerika kwa matangazo yasiyoegemea upande wowote, wakati nchi hiyo ikikabiliwa na mzozo unaoendelea wa kisiasa na wa kibinadamu.

“Ni muhimu sana kuendelea na matangazo hayo sasa, kuliko wakati mwingine wowote,” alisema afisa huyo mwandamizi.

Comments are closed.