Mkuu wa Shule Kisimiri Apewa Tuzo na Global Radio, Apokelewa Kishujaa (Picha +Video)
MKUU wa Shule ya Sekondari Kisimiri Arusha, Valentino Tarimo, Jumatano Julai 17, 2019 amekabidhiwa Tuzo ya Shukrani baada ya shule yake kuibuka kidedea kwa kufaulisha na kuwa ya kwanza nchini katika matokeo ya Kidato cha Sita mwaka huu.
Mwalimu Tarimo amekabidhiwa Tuzo ya Shukrani na Meneja Mkuu wa Global Group, Abdallah Mrisho kwa niaba ya Global Radio leo baada ya kupokelewa kishujaa na wafanyakazi wa kampuni ya Global Group alipofika ofisini kwao kufuatia mwaliko aliopewa na uongozi wa kampuni hiyo.
Meneja Mrisho alimsifu Tarimo na timu yake kwa kuwafanya wanafunzi hao kuongoza katika ufaulu kitaifa na kuifanya shule yao kuwa ya kwanza.
Mwalimu huyo aliyealikwa jijini Dar es Salaam na kituo cha redio ya mtandaoni inayokuja kasi nchini ya +255 Global Radio, alishukuru familia ya Global kwa kutambua kazi wanayoifanya ya kuelimisha wanafunzi.
Matokeo ya shule hii, yamefungua ukurasa mpya na kuzibeba shule za kata za serikali ambazo kwa muda mrefu zimekuwa hazionyeshi kufanya vizuri.
Kwa mujibu wa Tarimo, walimu wanaofundisha shule hiyo ni kawaida kwao kufanya vizuri katika kufaulisha.
Katika ziara hiyo Tarimo alifuatana na Mwalimu wa Taaluma, Eliutheo Severine na mwanafunzi wa kiume aliyefanya vizuri katika masomo ya sayansi, Herman Kamugisha.
Katika matokeo ya mtihani yaliyotangazwa hivi karibuni na Katibu Mkuu wa Baraza la Mitihani la Taifa, Dk. Charles Msonde, licha ya shule hiyo kuongoza kwa matokeo mazuri, bado hayajakata kiu ya Mkuu wa Shule Mwalimu Tarimo na walimu wenzake kufanya vizuri zaidi.
Stori na Elvan Stambuli
Comments are closed.