The House of Favourite Newspapers

 Mkwasa aweka rekodi ya kibabe Ligi Kuu Bara

0

 

 

KOCHA Mkuu wa Ruvu Shooting, Charles Boniface Mkwasa ‘Master’, ameweka rekodi ya kuwa kocha pekee mzawa aliyefanikiwa kukiongoza kikosi chake kukamatia moja ya nafasi tano za juu kwenye msimamo wa ligi, huku pia akiwa kocha pekee mzawa aliyefanikiwa kutwaa tuzo ya kocha bora wa mwezi mpaka sasa.

Mkwasa ambaye juzi Jumamosi alikiongoza kikosi chake kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mabatini, Pwani, ameiongoza Ruvu kwenye michezo 17 ya ligi msimu huu na kujikusanyia pointi 28 wakiwa kwenye nafasi ya nne.

Nafasi ya kwanza kwenye msimamo inakamatiwa na Yanga yenye pointi 44 ikiongozwa na Mrundi, Cedric Kaze, Simba iliyo chini ya Mbelgiji, Sven Vandenbroeck wako katika nafasi ya pili na pointi zao 35.

Azam ya George Lwandamina wao wanakamatia nafasi ya tatu na pointi zao 32 huku nafasi ya tano ikienda kwa Mkenya Francis Baraza anayeiongoza Biashara United yenye pointi 26.

Mkwasa pia amefanikiwa kutwaa tuzo ya kocha bora wa mwezi Novemba akiwashinda Mecky Maxime wa Kagera Sugar na Fulgence Novatus wa Gwambina alioingia nao fainali hivyo kuwa kocha mzawa pekee aliyefanikiwa kufanya hivyo.

Mkwasa alitwaa tuzo hiyo baada ya kuiongoza Ruvu Shooting kukwea kutoka nafasi ya 10 hadi ya nne kwenye msimamo wa ligi.

 

JOEL THOMAS,

Dar es Salaam

Leave A Reply