MBUNGE wa Ulanga, Goodluck Mlinga (CCM) ameomba mwongozo bungeni akihoji sababu ya serikali kutoa mipira ya kiume (kondomu) bure badala ya kugawa taulo za kike bure kwa wanafunzi.
Mlinga ameomba mwongozo huo leo Mei 22 bungeni mara baada ya kumalizika kwa kipindi cha maswali na majibu.
“Mheshimiwa Spika lazima tuwe wakweli ukiangalia ufaulu idadi kubwa inayofeli ni watoto wa kike hasa kutoka maeneo ya vijiji na kitendo cha kufeli ni kutokana na kutohudhuria vizuri masomo pindi wanapokuwa katika siku zao za hedhi. Mheshimiwa Spika, bunge limekuwa likipiga kelele ni namna gani ya kuwasaidia watoto wa kike wapate pedi za kike bure.
“Lakini tumeshuhudia serikali ikitoa vifaa tiba bure katika makundi mbalimbali ili kuwasaidia kuepuka magonjwa mbalimbali kwa mfano tumeshuhudia ikitoa ARV, dawa za TB bure. Mheshimiwa Spika, Serikali inagawa mipira ya kiume bure, ina maana Serikali yetu inawapa kipaumbele wazinifu na kuwaacha wanafunzi? Mheshimiwa Spika naomba mwongozo wako ni kwa nini isitoe pedi za kike bure,” amehoji Mlinga.
Akijibu, Spika amesema ni wakati muafaka wa serikali kuzungumza na bunge kuhusu hali hiyo.
Comments are closed.