MNADHIMU Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania, Mohamed Yacoub amefunga rasmi Mashindano ya Mchezo wa Golf ya Mkuu wa Majeshi ‘NMB CDF trophy 2019’ kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi, huku Benki ya NMB ikiahidi kuendelea kudhamini mashindano hayo.
Akizungumza jana katika viwanja vya Club ya Golf Lugalo jijini Dar es Salaam, Mnadhimu Mkuu JWTZ, Luteni Jenerali Yacoub ameishukuru Benki ya NMB kwa kuendelea kudhamini mashindano hayo, hivyo jeshi litaendelea kushirikiana na benki hiyo.
Aliwataka majenerali wa jeshi na wananchi wengine kuupenda na kuucheza mchezo wa golf na kuachana na mawazo ya baadhi ya watu wanaoamini kwamba mchezo huo ni wamatajiri pekee.
Awali akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Idara ya Wateja Wakubwa na Serikali wa Benki ya NMB- Filbert Mponzi alisema NMB ni wadau wakubwa wa Jeshi la Wananchi hivyo, itaendelea kusaidia mchezo wa golf hasa mashindano ya Club ya Mchezo wa Golf Lugalo ya jijini Dar es Salaam.
Alisema katika udhamini wa mwaka huu Benki ya NMB imetoa udhamini wa pesa ya kununua vifaa mbalimbali pamoja na zawadi za washindi kunogesha mashindano hayo na itaendelea kufanya hivyo.
Aidha aliongeza kuwa, NMB ni wadau wa Serikali na wabia pia kibiashara na Serikali hivyo inaamini inastahili kulihudumia Jeshi. “Mtandao tulionao ni mkubwa zaidi nchini nzima, tuna matawi zaidi 220, mashine za ATM zaidi ya 800 ambazo zingine zipo karibu na kambi za Jeshi la Wananchi na sasa tunaendelea kutanuka kupitia mtandao wa mawakala ambapo tuna zaidi ya mawakala 7000 maeneo mbalimbali ya nchini.” Alisema Bw. Mponzi.
Katika mashindano ya ‘NMB CDF trophy 2019’ mwaka huu yalioshirikisha makundi mbalimbali ya wachezaji nchini wakiwemo wa kulipwa takribani washindi 22 wamejinyakulia vikombe na zawadi anuai kulingana na nafasi walizoshinda.
Comments are closed.