Mo Atishia Kujiondoa Simba
TAARIFA zinaeleza kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Mohammed Dewji ‘Mo’, ameomba kujiondoa katika baadhi ya majukumu ya timu hiyo.
Taarifa hiyo imekuja siku moja baada ya mkutano wa aliyekuwa Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara kufunguka juu ya mambo mengi ambayo yamekuwa yakifanyika klabuni hapo pindi alipokua akihudumu.
Manara alifanya mkutano na waandishi wa habari juzi Jumatano katika Hoteli ya Serena ambapo katika mazungumzo yake alitoa tuhuma nzito kwa baadhi ya viongozi wa Simba akiwemo Mtendaji Mkuu, Barbara Gonzalez.
Licha ya kumtaja Barbara pia Manara kwenye mkutano huo mara kadhaa aliweza kumtaja Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Mohammed Dewji ‘Mo’. Kwa mujibu wa taarifa ilizozipata gazeti hili, Mo ameomba baadhi ya majukumu yake kama Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, yafanywe na makamu wake, Salim Abdallah ‘Try Again’.
“Mo ameomba kuondoka klabuni na kuomba baadhi ya majukumu yake kufanywa na makamu wake, Try Again kutokana na kukamilisha vitu vyote ambavyo vinahitajika.“
Ameona baadhi ya maamuzi mengi ya vikao vya bodi vifanywe na Try Again, tofauti na yeye alivyokuwa akifanya hapo awali huku kwa sasa Mo akiomba kuhusika mara chache kama mwenyekiti,” alisema mtoa taarifa wetu aliye karibu na tajiri huyo.
Championi Ijumaa, lilipomtafuta Mwenyekiti wa Simba, Murtaza Mangungu, alisema hawezi kuzungumzia taarifa hiyo.“Mimi siwezi kuzungumzia taarifa ambayo imewekwa mtandaoni labda iwe imewekwa kwenye ukurasa wa Klabu ya Simba, Mo au mimi.“Taarifa hizo zingewekwa kwenye kurasa hizo ningezungumzia ila kwa sasa siwezi kuzungumza juu ya jambo hilo,” alisema Mangungu.
Stori: LEEN ESSAU, Dar es Salaam