The House of Favourite Newspapers

Mo Dewji Aongeza Mzuka Simba

0

RAIS wa Heshima wa Klabu ya Simba, Mohamed Dewji ‘Mo’ ameongeza mzuka kwa wachezaji na benchi la ufundi la timu hiyo kuelekea mchezo wa leo Jumapili wa Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya RS Berkane baada ya kusema kuna bonasi nzuri ameiweka ili timu ishinde.

 

Leo Jumapili, Simba watakuwa wenyeji wa Simba katika mchezo huo wa Kundi D utakaochezwa Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Simba itaingia uwanjani ikiwa na kumbukumbu ya kufungwa mabao 2-0 dhidi ya RS Berkane katika mchezo uliopigwa Morocco.

Akizungumzia kile anachokiona kuelekea mchezo huo wa leo, Mo Dewji amesema: “RS Berkane ni timu nzuri, tumeona walivyocheza kule kwao ingawa hali ya hewa ya baridi kule ni tofauti na kwetu. Huku mechi itachezwa kwenye joto kali.

 

“Lakini pia wale ni wazuri katika mipira iliyokufa, naamini kocha (Pablo Franco) ni mzoefu na amewaandaa wachezaji kukabiliana na wapinzani wetu hao.

 

“Ninaamini kwa mapenzi ya Mungu tutashinda, hizi pointi tatu kwetu ni muhimu sana, moyo wangu unaniambia tutafanikiwa, ni muhimu timu kama Simba iendelee kufanya vizuri katika michuano ya kimataifa ili timu zingine nazo zipate nafasi ya kushiriki.

 

“Nina imani na benchi la ufundi, wachezaji na viongozi kwamba wanajituma, hivyo Imani yangu siku hiyo tutashinda.

“Wachezaji nawapenda sana, kabla ya mechi huwa namtumia mmoja mmoja kuwatakia mchezo mwema. Watuletee furaha, mimi mwenyewe Simba isipofanya vizuri naumwa, lakini pia nafikiria mamilioni ya Watanzania.”

 

KUHUSU BONASI ZA MECHI

Simba imekuwa na utaratibu wa kutoa bonasi kwa wachezaji wake kama motisha ya kupata ushindi ambapo inatajwa kwamba katika michuano ya kimataifa msimu huu, wamekuwa wakitoa si chini ya dola laki moja ambayo ni zaidi ya shilingi milioni 230 za Kitanzania.

 

Kuhusu bonasi hizo, Mo Dewji amefafanua kwa kusema: “Unajua sisi tumetoa bonasi ambayo hatuwezi kuitaja, mimi mwenyewe nimetoa bonasi, kabla ya kuingia katika mashindano haya (Kombe la Shirikisho Afrika) baada ya kutolewa Ligi ya Mabingwa, nilikaa nao tukazungumza, katika kila mechi kuna bonasi na baada ya kufuzu kuna bonasi, hilo linaenda vizuri sana.”

 

ISHU YA USAJILI

Mo Dewji amegusia usajili wa Simba kuelekea msimu ujao ambapo amebainisha kwamba, watasajili wachezaji wenye uwezo mkubwa.

Miongoni mwa wachezaji aliowatolea ufafanuzi ni washambuliaji, Moses Phiri raia wa Zambia na Mnigeria, Victorien Adebayor.

 

Phiri anayecheza Zanaco ya Zambia, inaelezwa kwamba, tayari amesaini mkataba wa awali na Simba, huku Adebayor anayekipiga US Gendermarie ya Niger, mazungumzo yameshaanza na mchezaji mwenyewe kuonesha nia ya kujiunga na Simba.

 

Akizungumzia usajili wa Adebayor, Mo Dewji alisema: “Ni mchezaji mzuri, lakini yeye mwenyewe ana hamu ya kuja kucheza Simba, kwa hiyo kamati ya usajili wameshaanza kuongea naye, kama makubaliano yatafikiwa anaweza kucheza Simba msimu ujao.

 

“Mambo ya usajili lazima yafanywe kwa akili kubwa na siri kubwa. Kwenye miaka hii minne tumejifunza mengi sana, naomba mtuamini kwamba hao wachezaji (Adebayor na Phiri) tunawafuatilia kwa karibu, kwa hiyo muda ukifika tutawaambia.

 

“Tuna kamati ambayo ipo inawafuatilia wachezaji ambao watasajiliwa. Tunajua kuhusu kufeli hasa kwa wachezaji, hilo halipo hapa kwetu pekee, hata Ulaya ipo hivyo, kuna wachezaji wanasajiliwa lakini wanashindwa kufanya vizuri, hivyo ishu ya mchezaji kusajiliwa kisha akafeli, ni jambo la kawaida.”

Leave A Reply