The House of Favourite Newspapers

Mo Dewji Kuwafanyia Kufuru Vita

0

 

PAMOJA na uongozi wa Klabu ya Simba kupeleka maombi kwa Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) ya kuomba mchezo wao dhidi ya na AS Vita ya DR Congo, usogezwe mbele hadi Aprili 4, mwaka huu, tayari bosi wao ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa klabu hiyo, Mohamed Dewji ‘MO’, ametoa ahadi ya kibabe kwa wachezaji wake ambapo amesema endapo kwenye mchezo huo watawafunga atatoa Sh milioni 500.

 

Kwenye michezo iliyopita Mo Dewji alitoa ahadi kama hizo, ambapo mchezo wa kwanza wa Simba na AS Vita kule Kinshasa, alitoa Sh 100m, lakini kwenye mchezo na Al Ahly ya Misri alitoa Sh 500m, wakati kwenye mchezo dhidi ya Al Merreikh ya Sudan ule wa kwanza alitoa Sh 250m na huu wa pili pia akatoa kiasi sawa na hicho.

Chanzo chetu makini kimeliambia Championi Ijumaa kuwa, mchezo wa Simba na AS Vita awali ulitakiwa kupigwa Aprili 2, mwaka huu jambo ambalo Simba wameomba kusogezwa mbele hadi hiyo Aprili 4, ambapo Mo yeye amesema kuwa kama watafanikiwa kupata pointi tatu kwenye Uwanja wa Mkapa atatoa kiasi hicho cha fedha kama motisha kwa benchi la ufundi na wachezaji.

 

“Bosi wetu amepania kumaliza mchezo mapema, hivyo amewataka wachezaji kwenye mchezo wetu na AS Vita hapa nyumbani, kuhakikisha wanapambana kupata pointi tatu ili tunapoenda kurudiana na Al Ahly kule Misri twende kucheza tukiwa tayari tumeshavuka, hivyo ameahidi kutoa kiasi cha dola laki mbili, ambazo ni sawa na zaidi ya milioni 500,” kilisema chanzo hicho.

 

GOMES AWATOLEA NENO VITA

Wakati huohuo, Kocha Mkuu wa Simba, Didier Gomes amebainisha wazi kwamba wanatakiwa kucheza kwa akili katika mechi yao na AS Vita kwa kuwa ndiyo ambayo itawapa uhakika wa wao kutinga katika Hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Kocha huyo ameongeza kwamba anajua bado hawajamaliza kazi yao katika michuano hiyo licha ya kwamba hadi sasa wanaongoza katika kundi lao wakiwa na pointi 10.

 

Simba ndiyo vinara wa Kundi A katika Ligi ya Mabingwa Afrika wakiwa na pointi 10 huku wakibakisha mechi mbili dhidi ya Vita na Al Ahly.

Mechi ijayo Simba watacheza na Vita kwenye Uwanja wa Mkapa, Aprili 2, mwaka huu.Gomes ameliambia Championi Ijumaa kuwa katika mechi hiyo na Vita wanatakiwa kucheza vizuri zaidi kwa sababu ndiyo ambayo itakuwa imebeba tiketi ya wao kutinga hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.

 

“Tuna pointi 10 hadi sasa na pia tupo kileleni mwa msimamo, ila bado tuna mechi za kucheza mbele. Tunahitaji alama moja zaidi ya kwenda robo fainali.“Sasa tuko kwenye njia nzuri kwa sababu tumeshinda mechi tatu na sare moja ila kuna kitu tunatakiwa tukifanye kwenye mechi ijayo.

 

“Tunahitaji kucheza vizuri zaidi mbele ya AS Vita, kwa sababu ndiyo itatupa uhakika wa kwenda mbele au la, lakini nawajua Vita ni timu hatari hivyo tunatakiwa kuwa makini,” alimaliza Gomes.

MUSA MATEJA NA SAID ALLY

Leave A Reply