The House of Favourite Newspapers

MOBETO APIGA MIL 50 KWA MWEZI

DAR ES SALAAM: MUNGU akiamua kukupa atakupa tu! Baada ya kudharauliwa mno mitandaoni, hatimaye staa ‘grade one’ ambaye pia ni mwanamitindo na msanii wa Bongo Fleva, Hamisa Mobeto, maisha yameanza kumnyookea, Gazeti la Ijumaa limedokezwa.  Habari ya uhakika ni kwamba, Mobeto kwa sasa anapiga zaidi ya shilingi milioni 50 kwa mwezi. Mobeto ambaye ni mama wa watoto wawili mmoja akiwa amezaa na Mkurugenzi wa E-FM na TV-E, Francis Siza almaarufu, Majizo na mwingine amezaa na staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, kwa muda mrefu amekuwa akibezwa mitandaoni kama ni mtu wa kudanga. Mobeto amekuwa akionekana anategemea pesa za matunzo ya watoto kutoka kwa wanaume hao ili kutanua mjini.

TUJIUNGE NA MENEJA

Akizungumza na Gazeti la Ijumaa, meneja wa Mobeto, Maximilian Rioba ambaye amekuwa naye kwa muda wa mwezi sasa anasema kuwa, kwa sasa msanii huyo amekuwa akilamba madili mengi ndani ya muda mfupi. Max anasema hadi sasa Mobeto ameshalamba madili ya zaidi ya shilingi milioni 50 kwa mwezi mmoja tu.

“Mimi na yeye tuna makubaliano kwamba anataka kuona anakuwa zaidi, ndiyo maana mnaona siku za hivi karibuni tumefanya vitu vinayoonekana kuna matokeo mazuri. “Hadi sasa ndani ya mwezi tu, Mobeto ameshafanya madili matatu makubwa yenye makadirio ya zaidi ya shilingi milioni 50 na hiyo ni kwa mwezi tu tangu niwe naye,” anasema Rioba ambaye pia ni mwanamuziki mkali wa RNB Bongo.

ANAINGIZAJE PESA

“Tumetengeneza usawa wa gharama kutokana na kazi anayotaka mteja. Unataka akutangazie kwenye mitandao yake ya kijamii, awe balozi wako, aje kwenye shoo yako kama sehemu ya kuonekana (appearance) au kupafomu, hapo tunaangalia gharama, tunaingia makubaliano na hii nikwambie kwa uwazi tangu nimekuwa naye hajawahi kupata pesa hizi kwa kipindi kifupi hapo nyuma. Mobeto sasa ni brand (bidhaa) kubwa mno.”

MADILI MENGINE YAJA

Meneja Maxi anasema kwamba, kuna uwezekano mkubwa wa kufanya madili mengi na watu wasione kwamba Mobeto atakuwa kwenye muziki tu, bali atapata mengi kupitia vitu vyake vingine zaidi ya kumi.

“Hamisa (Mobeto) anaweza kufanya vitu vingi vikubwa si muziki tu, sawa muziki anapenda tu, lakini madili yake yapo kwenye vitu zaidi ya kumi kama vile filamu, mitindo na shoo za TV. Kwa hiyo mimi kazi yangu ni kuangalia jinsi ya kumtengeneza zaidi na kuingiza kipato. Huwezi kuamini, lakini silali, nafikiria kumtengeneza Hamisa (Mobeto) ili siku akifikia malengo kila mmoja ashangae.”

KUTIKISA AFRIKA

Mbali na kupata madili hayo, Mobeto amepata dili la kufanya muziki na staa mkubwa kutoka Afrika (jina linahifadhiwa) na kinachosubiriwa ni kutikisa nchi. “Mobeto ndiye aliyeanza kuwasiliana na staa huyo namba moja kwa Afrika ambaye alishangaa kumsikia kwa kuwa anaona kazi zake anazozifanya hivyo akaniunganisha naye, nikafanya mawasiliano. Tumefikia vizuri na muda wowote tunatikisa nchi,” anasema Maxi ambaye pia ni prodyuza mkali.

AMSIFIA MOBETO

Maxi anasema kuwa, kabla hajakutana na Mobeto kuna mtu alimwambia akiweza kufanya kazi naye atafika mbali sana, akamfuata na kumwambia afanye naye biashara kama anaweza. “Mobeto hachelewi kwenye makubaliano hata siku moja, hawezi kuacha kupokea simu yako na hata nikimwambia tunaenda kwenye madili yeye atakuwa wa kwanza kufika. “Hamisa (Mobeto) havuti sigara wala hanywi pombe tofauti na mastaa wengine ambao lazima utasumbuana nao kuanzia kwenye ulevi hadi kwenda kwenye madili.

“Nimekaa naye kwa mwezi tu, nimemuona ni wa tofauti na mastaa wengi hata pale tunapokubaliana dili na kampuni yupo tayari kuridhika na kusema tuchukue tu. Kifupi tunavyofanya kazi ni tofauti inafikia wakati wa kuchukua pesa anakwambia chukua zaidi huyo ndiye Hamisa (Mobeto.”

KUHUSU KUCHANGISHIWA PESA

Meneja huyo alisema kwa sasa hamuoni Mobeto akienda tena kuomba pesa japokuwa suala lake na wazazi wenzake hayo ni mambo yao binafsi kutokana na walivyokubaliana. “Naangalia maisha ya kumtengeneza Hamisa (Mobeto), simuoni kabisa akiishiwa kutokana na madili anayoendelea kuyapata.”

KINACHOWAANGUSHA MASTAA WENGINE

Maxi aliiambia Gazeti la Ijumaa kuwa tangu ametangaza kuwa meneja wa Mobeto simu zimekuwa nyingi kutoka kwa mastaa wakubwa japokuwa ni ngumu kufanya kazi nao. “Kuna mastaa wana mashabiki zaidi ya milioni tatu mitandaoni, lakini nidhamu hawana, siwezi kuwa nao kwa sababu ninachofanya ni muongozo tu tabia ni yako. Ni wachache sana nchini wenye hicho kitu na ndiyo kinachowafelisha mastaa wengi Bongo.”

MADILI YA MOBETO

Mobeto hadi sasa ameshalamba madili mengi yakiwemo ya nywele (Prima), kampuni ya vifaa vya jikoni na bafuni ya Dar Ceramica, Kampuni ya GSM inayodili na kuuza nguo, Multi-Choice Tanzania na nyinginezo ikiwemo kampuni moja ya Wachina

 

Stori: ANDREW CARLOS NA SHAMUMA AWADHI, IJUMAA

Comments are closed.