The House of Favourite Newspapers

Mohammed Iqbal Dar: Mbunifu wa jina la Tanzania

1

Katika safu yetu ya wiki hii ya Mleta Mabadiliko tunaye Mohammed Iqbal Dar ambaye ndiye aliyeleta mabadiliko makubwa la jina la nchi, kutoka Tanganyika na kuwa Tanzania baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.

Mohammed Iqbal Dar ndiye aliyebuni jina zuri la Tanzania. Vijana wengi pengine hata wazee hawamjui wala kusoma historia yake kwani haifahamiki.
Mwandishi mmoja wa Redio Safari ya Mtwara Alphonce Tonny Kapelah alipata bahati ya kuonana ana kwa ana na kuzungumza na Mohammed Iqbal Dar akajieleza:
Swali: Uliingiaje katika shindano la kubuni jina la nchi?
Jibu: Siku moja nilikuwa maktaba nikijisoma Gazeti la Tanganyika Standard ambalo siku hizi linaitwa Daily News, mikaona tangazo lililosema: “Muungano wa Tanganyika na Zanzibar unafahamika kama Republic of Tanganyika and Zanzibar jina likaonekana refu sana. Kwa hiyo wananchi wote mnaombwa kushiriki kwenye shindano la kupendekeza jina moja litakalozitaja nchi zote mbili yaani Tanganyika na Zanzibar.”
Swali: Baada ya kuona tangazo hilo ukafanyaje?
Jibu: Niliamua kuingia kwenye shindano hilo.

Swali: Ulianzaanzaje kubuni jina linalofaa?
Jibu: Nilichukua karatasi nikaandika kwanza Bismillah Raahman Rahimu hii ni kutokana na imani ya dini yangu. Baada ya hapo nikaandika jina la Tanganyika kisha nikaandika Zanzibar halafu nikaandika jina langu la Iqbal halafu nikaandika jina la Jumuiya yangu ya kidini ya Ahmadiya. Baada ya hapo nikamrudia tena Mwenyezi Mungu, nikamuomba anisaidie ili nipate jina zuri kutoka katika majina hayo niliyokuwa nimeandika. Baada ya hapo nilichukua herufi tatu kutoka jina la nchi ya Tanganyika yaani TAN na kwa upande wa Zanzibar nikachukua herufi tatu za mwanzo ZAN, kisha anikaunganisha nikapata jina TANZAN.
Swali: Mbona halijakamilika?
Jibu: Nami niligundua kuwa halijakamilika hivyo nikachukua herufi ya kwanza ya jina langu ambayo ni herufi I katika jina langu la Iqbal kisha nikachukua herufi ya kwanza A ya jina la dini yangu yaani Ahmadiya. Niliandika jina la awali la TANZAN nikaunga na herufi hizo likawa TANZANIA nikaona ni jina kamili tena zuri.

Swali: Ulipopata jina hilo la Tanzania ulifanyeje?
Jibu: Kabla ya kulipeleka kunakohusika serikalini nilifanya utafiti mdogo na kugundua kuwa nchi nyingi za Afrika majina yao yanaishia na IA kwa mfano EthiopIA, ZambIA, NigerIA, TunisIA, SomalIA, GambIA, NamibIA, LiberIA, MauritanIA. Baada ya utafiti huo nikapendekeza na kuamua kwamba jina TANZANIA ndilo litumike kuwakilisha nchi hizi mbili yaani Tanganyika na Zanzibar. Kwa maana hiyo jina TANZANIA limezaliwa kutoka katika majina manne ambayo ni Tanganyika, Zanzibar, Iqbal na Ahmadiyya.

Swali: Ikawaje?
Jibu: Baada ya kujiridhisha kuwa jina hilo linafaa nikalituma kwenye kamati ya kuratibu shindano. Baada ya muda mwingi kupita baba yangu Dk. Dar alipokea barua nzito kutoka iliyokuwa Wizara ya Habari na Utalii ilisomeka kama ifuatavyo:
“Utakumbuka kuwa miezi michache iliyopita ulituandikia kutupa ushauri kuhusu jina jipya la Muungano wa Tanganyika na Zanzibar….ili iitwe Tanzania.
“Nafurahi kukuarifu kuwa mshirikiane zawadi ya sh.200 iliyoahidiwa na leo nakuletea cheki ya sh.12/50 ikiwa ni hisa yako katika zile sh. 200.
Nashukuru sana kwa jitihada ya kufikiri jina la jamhuri yetu.”
Barua ikasainiwa na Idrisa Abdul Wakil Waziri wa Habari na utalii kipindi hicho.
Swali: Kwani washiriki mlikuwa wangapi?
Jibu: Tulikuwa watu 16 lakini mimi nikaibuka mshindi lakini alijitokeza mtu mmoja, Yusufal Pir Mohammed aliyedai naye alishinda, hata hivyo, alikosa sifa baada ya kushindwa kutoa barua ya uthibitisho na kupongezwa kama nilivyoandikiwa mimi na serikali, sasa nikapewa cheki ya shilingi 200 na zawadi ya ngao. Nilileta mabadiliko makubwa sana ya jina jipya. Ninachosikitika ni kuwa mchango wangu bado Watanzania hawauthamini lakini mimi naipenda Tanzania na najivunia kuwa Mtanzania ila naamini kuwa siku moja ukweli utajulikana.
Swali: Hivi sasa unaishi wapi?
Jibu: Kwa sasa naishi Uingereza kwa kuwa huko ndiko nilipata kazi eneo la Birmigham b35 6ps UK, Dar es Salaam House, 18 Turnhouse Road.
Swali: Unaweza kutueleza historia yako kifupi?
Jibu: Mimi Mohamed Igibal Dar ni Mtanzania mwenye asili ya Kihindi, nilizaliwa mkoani Tanga mwaka 1944. Baba yangu alikuwa daktari wa binadamu mkoani Morogoro alikuwa anaitwa Dk. Tadar na alihamia Tanganyika kutoka India mwaka 1930. Nilipata elimu ya msingi mkoani Morogoro katika Shule ya Msingi H.H Agha Khan, kwa sasa ni shule ya serikali.
Baadaye nilijiunga na Shule ya Mzumbe nikasoma kidato cha kwanza mpaka cha sita.

1 Comment
  1. Elias Emmanuel Magere says

    Hiyo ni elimu haswaa, kunahitajika uchapishe picha yake kwani wengi hatukujua hilo, asante

Leave A Reply