The House of Favourite Newspapers

MPENZI WANGU SARAFINA-12

0

Richard akaingia nchini Marekani, moyo wake ulikuwa kwenye maumivu makali, hakuamini kama alimkosa msichana ambaye alimpenda kwa moyo wa dhati, msichana ambaye kila siku katika maisha yake alimpa nafasi ya kwanza moyoni mwake.

Alilia na kuhuzunika, alimpenda Sarafina kwa mapenzi ya dhati. Hakukuwa na mtu aliyejua ni kwa jinsi gani alimpenda msichana huyo. Alijaribu kumwambia sana lakini hakueleweka, alionekana muongo kama wanaume wengine.

Nchini Marekani hakutaka kujiingiza kwenye uhusiano na msichana yeyote yule, moyo wake uliamini kwamba kuna siku angekutana na msichana Sarafina, hata kama angekuwa amezaa, kwake kuishi na msichana mwenye mtoto halikuwa na tatizo lolote lile, alichokuwa akikiangalia ni moyo wake,e alitaka uridhike, ufurahie kwa kile kilichokuwa kimetokea.

Baada ya kukaa hotelini kwa siku mbili huku akimfikiria Sarafina, hatimaye siku iliyofuata ilikuwa ni kwenda katika Chuo cha Kikuu cha Mississippi na kuanza masomo chuoni hapo.

Akili yake ilitulia, hakutaka kumfikiria msichana yeyote yule, aliyekuwa akimfikiria kwa wakati huo alikuwa msichana Sarafina tu ambaye hakujua alikuwa mahali gani. Maisha yalisonga chuoni hapo, uwezo wake haukuwa mkubwa sana, ulikuwa wa kawaida ila kutokana na ucheshi wake, watu wengi wakatamani sana kuzungumza nayee.

Alikuwa akijua mambo mengi, alisoma vitu vingi mno, alizijua historia nyingi kichwani mwake kiasi kwamba wanafunzi chuoni hapo wakampa jina la Encyclopedia (Kitabu cha Hifadhi Matukio Mengi Yaliyotokea Duniani).

Watu wengi walipenda kuzungumza naye, kuwa karibu na watu wengine, kubadilishana nao mawazo hatimaye akaanza kumsahau msichana Sarafina. Akawa akifanya mambo yake na watu wengine, yale maumivu aliyokuwa nayo kipindi cha nyuma yakapotea kabisa kitu ambacho kilimpa furaha na amani moyoni mwake.

Aliendelea kuwafurahisha watu wengi kuhusu matukio mengi yaliyopita kama kutengenezwa bustani inayoelea, mpiganaji wa Kihispania, CID jinsi alivyokuwa akiitetea Dini ya Kiislamu, mchoro wa Mona Lisa ulivyotumia miaka zaidi ya kumi kuchorwa, kuibwa na kupatikana, maisha ya mwanamashairi William Shakespear, mwanamke aliyekadiriwa kuwa na uzuri kuliko wote, Cleopatra kiasi cha kuolewa na ndugu zake wawili akiwemo mwanaume mwingine, Mark Antony.

Kila alichokuwa akiwaambia watu walibaki wakimshangaa, hawakuamini kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akijua vitu vingi kichwani mwake. Wanawake wakaanza kumpenda na mtu ambaye alimtamani kila siku alikuwa msichana aliyeitwa Bianca Massawe.

Huyu alikuwa msichana mrembo, aliyekuwa akivutia kwa sura ambaye naye alikuwa mwaka wa kwanza chuoni hapo. ALipenda kuwa na Richard kila sehemu alipokuwa, mara nyingi alikuwa akimfuata na kuzungumza naye, alimzoea na kila siku alikuwa akijiuliza ni kwa namna gani angeweza kumwambia jinsi moyo wake ulivyokuwa ukijisikia juu yake.

Alivumilia, aliuona ugumu mbele yake kwani kila alipokuwa akiingizia stori za kimapenzi, Richard alimtoa nje ya mada na kumuingizia mambo mengine kabisa.

“Richard, mapenzi yanauma sana,” alisema Bianca huku akimwangalia Richard.

“Najua!”

“Moyo wangu unahisi kitu kimoja kizito sana juu yako,” alisema Bianca huku akimwangalia mwanaume huyo.

“Bianca! Hivi nilishawahi kukwambia kuhusu lile sanamu la Liberty liiloshika mwenge la hapo New York?” aliuliza Richard.

“Hapana!”

“Lile lilikuwa ni zawadi kutoka nchini Ufaransa. Yaani baada ya bifu kubwa la Ufaransa na Uingereza katika kutawala makoloni, Uingereza alipopigwa vita na Marekani na kuondoka Julai 4, mwaka 1776, Ufaransa ikafurahi na hivyo jamaa mmoja aliyeitwa Gustave Eiffel akauchora mchoro wa sanamu hilo na akalitengeneza kisha kupewa Marekani ambao wakaliweka Manhattan jijini New York kwenye kakisiwa kadogo tu. Ukifika tu utaliona, lipo karibu na Bandari ya New York,” alisema Richard mfululizo ili Bianca asimwambie kuhusu mapenzi.

“Sawa. Nashukuru kwa kuniongezea elimu. Turudi kwenye mada yetu kuhusu lile suala,” alisema Bianca.

“Halafu kuna kitu nilisahau kukwambia. Huyu jamaa aliyetengeneza lile sanamu la Liberty anayeitwa Gustave Eiffel ndiye aliyetengeneza ule mnara mkubwa pale Ufaransa unaoitwa Eiffel, ulipewa jina hilo kumuenzi,” alisema Richard, japokuwa alikuwa akiongea vitu vya maana lakini kwa Bianca viliingia sikio la kushoto na kutokea la kulia.

“Sawa. Kwa hiyo?”
“Nitazungumza na wewe. Ngoja nikasome kidogo. Nataka nijue mengi kuhusu Leonardo Da Vinci. Nikishakamilisha, nitakwambia,” alisema Richard, hapohapo akasimama na kuondoka zake.

Bianca akabaki akiwa amesimama tu, alichanganyikiwa, moyo wake uliuma, hakujua ni sababu gani iliyomfanya mwanaume huyo kutokutana kusikia chochote kuhusu mapenzi. Wakati mwingine alibaki akishangaa huku kichwa chake kikiwa na maswali mengi mno.

“Kwa nini hataki? Hajawahi kuwa na mwanamke? Kaumizwa au? Hapana! Nitahakikisha mpaka nampata!” alisema Bianca huku akionekana kupania haswa. Hakutaka kusikia lolote lile, alichokitaka ni kuwa na Richard tu.

****

Bado serikali ya Tanzania ilikuwa ikipambana kuhakikisha kwamba biashara ya madawa ya kulevya inateketezwa nchini. Kila mtu kwa wakati huo alikuwa akipambana, viongozi wengi walikamatwa na kufikishwa katika vituo mbalimbali vya polisi kwa ajili ya kuhojiwa kwa tuhuma za kujihusisha na madawa ya kulevya.

Kila siku vijana waliendelea kuharibika kwa kutumia madawa hayo. Serikali kwa kushirikiana na jeshi la polisi ilijitahidi kuchunguza kujua mahali madawa hayo yalipokuwa yakiingiziwa.

Waliwafahamu  watumiaji, hawakutaka kudili nao, walichokuwa wakikitaka ni kuwafahamu waingizaji kwani kama wangewabana hao basi ingekuwa rahisi kwao kuwafanya watumiaji kukosa unga na mwisho wa siku kupotea kabisa.

Kazi ilikuwa kubwa, walipokuwa wakizuia uingizaji kwa uwanja wa ndege, waingizaji waliingiza njia nyingine, maduka mengi ya Bureau De’Change yalikuwa yakitumiwa sana katika uingizaji huu.

Wafanyabiashara wakaanza kuagiza unga wa ngano kutoka nje na nafaka nyingine lakini ndani yake kulikuwa na unga huo haramu ambao kuuona tu ilikuwa kazi kubwa.

Wakati polisi wakiendelea na upelelezi wao wa kimyakimya, hawakujua kama muingizaji mkuu alikuwa Mzee Mpobela. Huyu alikuwa bilionea mkubwa, japokuwa alikuwa na biashara nyingi, kampuni lakini biashara yake nyingine kubwa ilikuwa ni usafirishaji wa madawa ya kulevya.

Aliwatumia vijana wengi katika biashara hiyo, aliwasafirisha kwa ndege na kufanya mipango yake katika viwanja vya ndege. Hakukuwa na aliyejua alichokuwa akikifanya lakini alikuwa ni mtu mwenye nguvu sana ambaye alipokuwa akiamua kufanya jambo fulani, alilifanya bila tatizo.

Alimpenda binti yake Gloria, kitendo cha mwanaume David kujitokeza kwa ajili ya kumuoa, aliridhika naye, aliahidi kugharamia kila kitu lakini mwisho wa siku mkewe aingie ndani ya ndoa.

“Nitagharamia kila kitu katika harusi yako na David. Unataka iwe lini?” aliuliza Mzee Mpobela.

“Miezi miwili ijayo!” alijibu Gloria.

“Basi usijali binti yangu!”

Aliwataarifu marafiki zake kwamba alikuwa akitarajia kuolewa na David. Kama alivyokuwa na furaha, hata marafiki zake walifurahi kwani kama hamu ya kuolewa, Gloria alikuwa nayo kubwa mno.

Upande wa pili biashara iliendelea kufanyika. Serikali ikatilia mkazo na mwisho wa siku watu waliokuwa wakitumwa kuingiza madawa hayo Tanzania wakawa wakikamatwa hovyo kitu kilichomfanya Mzee Mpobela kuchanganyikiwa.

“Tumebaki na vijana wangapi?” aliuliza Mzee Mpobela.

“Watatu!”
“Haiwezekani!”
“Ndiyo kiongozi. Watatu!”

“Nitafutieni vijana wengine wa kwenda Brazil,” alisema Mzee Mpobela.

Vijana wakatafutwa lakini walikosekana, kila mmoja aliogopa kwani kazi ya kuingiza unga ilikuwa ni ya hatari sana kipindi hicho ambacho serikali ilikuwa imechachamaa.

“Kama vijana wanaogopa, nitazungumza na David. Mzigo wa Brazil ni muhimu sana,” alisema Mzee Mpobela.

Hakutaka kuchelewa, haraka sana akampigia simu David na kuomba kuonana naye. Gloria hakutakiwa kufahamu kitu chochote kile, alimwambia kwamba kukutana nao iwe siri yao tu.

Hilo halikuwa na tatizo, baada ya dakika kadhaa wakaonana katika Hoteli ya Serena na kuanza kuzungumzia suala hilo. Mzee huyo alimwambia David kila kitu alichotaka kumwambia, akamtoa hofu kwamba kila kitu kingekwenda kama kilivyotakiwa kwenda.

Alihakikishiwa kulindwa kwa nguvu zote, hofu ikamuondoka moyoni na kumwambia mzee huyo kwamba alikuwa tayari kwenda kuchukua mzigo nchini Brazil.

“Nashukuru sana! Ila kuwa makini!” alisema Mzee Mpobela.

“Hakuna shida. Wewe niamini mimi kwamba nitauchukua mzigo na kukufikishia bila tatizo lolote. Hata uwanja wa ndege wakiweka polisi wote nchini Tanzania, mzigo utaingia tu,” alisema David huku akitoa tabasamu pana.

“Nashukuru sana mkwe wangu! Ukitoka huko, harusi inatakiwa kufanyika,” alisema Mzee Mpobela huku akiachia tabasamu pana usoni mwake.

“Ahsante sana kwa kunishirikisha katika jambo hili!” alisema David.

“Haina shida. Ila kumbuka ni siri! Usimwambie Gloria.”
“Haina shida.”
“Deal?”
“Deal!”

****

Malaika akaingia ndani ya kibanda chao, alimuona mama yake akiwa amelala chini, alikuwa kimya, alikuwa amefariki dunia, Malaika hakuwa na hofu, moyo wake ulimwambia kwamba mama yake alikuwa amelala hivyo angefanya kazi nyingine na baadaye kumuamsha.

Akaanza kuosha vyombo, kichwa chake kilikuwa na mawazo tele, hakujua kama alitakiwa kumwambia mama yake kutokana na ukatili aliokuwa amefanyiwa au la. Alipomaliza, akawasha moto na kuanza kupika.

Muda wote alikuwa akibubujikwa na machozi, bado aliendelea kusikia maumivu makali katikati ya mapaja yake. Alihisi kabisa kulikuwa na majimaji yakiteremka mpaka mapajani mwake.

Hakujua kama zilikuwa damu au majimaji ya kawaida. Kila wakati alikuwa akiyafuta machozi yake, kumbukumbu ya kile alichokuwa amefanyiwa kilirudi kichwani mwake, kilimuumiza kupita kawaida.

Alipomaliza kupika, akaweka sahani karibu na mama yake kisha kuanza kumuamsha. Alimuamsha kwa kumuita, Sarafina akawa kimya, akahisi kwamba inawezekana alikuwa amechoka sana hivyo kumgusa na kumtingisha.

Hali haikubadilika, bado Sarafina alikuwa kimya pale chini alipokuwa amelala. Malaika akashtuka, akahisi kwamba kuna kitu kilikuwa kimetokea, akazidi kumwamsha mama yake lakini hakuamka, mbaya zaidi kila alipokuwa akimsukuma huku, alikwenda bila kubisha chochote kile.

Akashtuka, mapigo ya moyo yakaanza kumuenda mbio, akahisi kwamba mama yake alikuwa amekufa, machozi yakaanza kumtoka na kutiririka mashavuni mwake. Akaupeleka mkono wake katika upande wa moyo wa mama yake, haukuwa ukidunda, ulikuwa umetulia, hapo akawa na uhakika kwamba mama yake alikuwa amekuga.

Aliumia mno, machozi yaliyokuwa yakimtoka, yakaongezeka, akalia kwa kumuita mama yake, hakuamini kilichokuwa kimetokea, mwanamke ambaye kila siku alikuwa akimthamini, aliyekuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati, leo hii alikuwa naye kimwili lakini kiroho hakuwa naye.

“Mama! Mama! Mama amkaaaa…” alisema Malaika kwa sauti huku akimwamsha mama yake.

“Mama usiniache, mama amka uniangalie, mama nimekuja, mama nimekupikia, amka ule, amka mama yangu, naomba usife, mama usiniache, mama, mama, mama, mama yafumbue macho yako, mtoto wako nimerudi mama, naomba usiniache mama, nitaishi na nani? Nani atanipenda? Nani atanijali? Mama amka mama,” alisema Malaika huku akiendelea kulia.

Sauti yake kali, kilio chake ndicho kikawaita watu wengine waliokuwa wakipita njia na kuingia humo ndani. Wakajua kwamba kulikuwa na tatizo, walipoingia, wakamkuta msichana huyo akimuamsha mama yake lakini hakuamka.

Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumtoa ndani na kumuweka nje huku mwanaume mwingine akimzuia kuingia ndani. Wanaume wale waliokuwa humo wakagundua kwamba mwanamke huyo alifariki dunia huku akinuka kuupita kawaida.

Walisikitika, hawakuamini kile walichokuwa wamekiona, kifuani mwa Sarafina, alikuwa ameoza, alitoa harufu kali hali ambayo wakati mwingine iliwafanya kuhisi kwamba mwanamke huyo alifariki muda mrefu na wakati huo alikuwa ameoza.

“Mbebeni tumpeleke hapo Amana,” alisema mwanaume mmoja na hivyo kumbeba.

Malaika alilia mno, alipiga kelele, kila mtu aliyekuwa akimwangalia aliona ni kwa jinsi gani msichana huyo alikuwa ameumia moyoni mwake. Mwili ukatolewa ndani ya kibanda kile na kisha kupelekwa katika Hospitali ya Amana ambao haikuwa mbali kutoka hapo walipokuwa.

Huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kumuona mama yake. Alisikitika mno, hakumfahamu baba yake, aliambiwa kwamba mwanaume huyo alifariki dunia miaka mingi iliyopita, kipindi ambacho alikuwa mdogo kabisa.

Baada ya kumzika mama yake katika Makaburi ya Mburahati, akaendelea kuishi maisha yake ya kuhangaika kutafuta chakula. Akahama kule alipokuwa akiishi na mama yake na kuhamia Mitaa ya Kariakoo.

Huko, akaungana na wenzake wengi waliokuwa wakiomba na kulala mitaani kila siku. Maisha yaliendelea kuwa ya shida mno, hakukuwa na nafuu hata kidogo. Si yeye tu aliyekosa chakula bali hata wenzake pia walikosa.

Wakati mwingine alikuwa akikaa peke yake na kumkumbuka mama yake, moyo wake ulimuuma kumpoteza mwanamke huyo ambaye kwake alikuwa kila kitu. Alihuzunika na kulia lakini machozi na huzuni zake hazikuweza kumrudisha mwanamke huyo duniani.

Japokuwa alikuwa mtoto wa mitaani lakini uzuri wake haukujificha, wavulana wengi waliokuwa wakimuona huko mitaani, walimpenda, walitamani sana kufanya naye mapenzi kwani alikuwa akilipa na hata kifua chake kilionyesha kabisa kuwa kibichi.

Kila siku usiku alikuwa akilala na wenzake, watoto wa mitaani zaidi ya ishirini. Walikuwa wakijikusanya katika maduka mbalimbali hapo Kariakoo na kulala pamoja. Hayo yalikuwa maisha yao ya kila siku, baridi lilikuwa likiwapiga mno, mvua iliponyesha, maji yaliwalowanisha, kwa kifupi, mbali na mateso yote waliyokuwa wakipata hawakuweza kupata msaada wowote ule.

“Amka…amka,” alisikia sauti ya mwanaume mmoja, alikuwa amemfuata pale alipokuwa amelala. Malaika akashtuka kutoka usingizini na macho yake kukutana na mwanaume mmoja, alimjua, alikuwa Ibrahim, kijana mwenzake wa mitaani ambaye alikuwa akizunguka naye mitaani kuombaomba fedha.

“Nini?” aliuliza Malaika.

Ibrahim hakutaka kusikia kitu chochote kile, baridi lilikuwa kali na kitu pekee alichokuwa akikihitaji mahali hapo ni ngono tu. Alimtamani sana Malaika, kwake, kila alipokuwa akimwangalia alimtamani kupita kawaida.

Hakutaka kumuona akichukuliwa na mwanaume mwingine, hakutaka kuona binti huyo mrembo akitembea na mwanaume mwingine, alimtamani na kwake alionekana kama mwanamke wake wa ndoto.

Alichokihitaji usiku huo ni kufanya naye ngono tu. Hakutaka kusikia kitu chochote kile, alimtamani kwa kipindi kirefu na muda huo ndiyo ulikuwa wa kufanya naye mapenzi. Malaika aliogopa, aliyakumbuka maumivu aliyoyasikia kipindi cha kwanza alipobakwa, hakutaka kuona hilo likitokea, alitaka kuona akiishi maisha mazuri na si kubakwa kama ilivyokuwa kipindi cha kwanza.

“Hapana! Sitakiiiii! Sitakiiiiiii!” alisema Malaika huku akijaribu kumtoa Ibrahim katika mwili wake.

“Nimesema tulia. Nitakuchinja,” alisema Ibrahim kwa sauti ya kitemi huku akimuwekea kisu Malaika shingoni mwake.

Malaika akaogopa, moyo wake ukajawa hofu, akajua kwamba kama angepiga kelele basi angeweza kuchinjwa kama alivyoambiwa. Haraka sana Ibrahim akaanza kumvua nguo. Hakukuwa na mtu aliyeona, wote walikuwa wamelala fofofo kutokana na kuchoka sana.

Alipohakikisha amemvua sketi Malaika, na yeye akafungua zipu ya suruali yake na kuanza kumbaka msichana huo mahali hapo. Malaika alilia mno, hakuamini kama alikuwa akibakwa kwa mara ya pili.

Hakusikia maumivu makubwa kama kipindi cha nyuma, alijitahidi kutaka kupiga kelele lakini kiganja cha Ibrahim kiliufunika mdomo wake vilivyo. Mwanaume huyo alichukua dakika kumi nzima kumbaka, alipomaliza, akajiweka pembeni na kufunga zipu ya suruali yake.

“Na kesho tena,” alisema Ibrahim huku akimwangalia Malaika aliyekuwa akilia kwa kuugumia kwa maumivu makali.

 

Je, nini kitaendelea?
Tukutane Alhamisi hapahapa.

Leave A Reply