Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dkt. Aneth Komba amesema kuwa, ujio wa mradi wa “Korea e- learning Improvement Cooperation (KLIC) utasaidia kuboresha Elimu nchini katika eneo la TEHAMA.
Dkt. Komba amesema hayo leo Novemba 6, 2023 alipoambatana na Gavana wa Gwangju Metropolitan , Mhe. Lee Jeong na Wataalamu wengine kutoka Korea Kusini wakikagua mradi huo katika shule ya msingi Tegeta A Jijini ,Dar es Salaam.
Dkt. Komba amesema kuwa mradi huo umekuja kwa wakati muafaka ambapo Serikali tayari imetangaza Sera mpya ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 Toleo la 2023 ambapo kuanzia mwaka 2024 mtaala mpya unatarajiwa kuanza kutumika.
Ameendelea kusisitiza Mtaala huo umetilia mkazo matumizi ya TEHAMA katika ufundishaji na ujifunzaji.
Aidha, Dkt. Komba amewashukuru Gwangju Metropolitan ya Korea Kusini kupitia GERIS kwa kufadhili mradi huo kwa kuleta vifaa mbalimbali ikiwemo kompyuta pamoja na kutoa mafunzo kwa wataalamu namna ya kutumia vifaa hivyo.
Kwa upande wake, Gavana wa Gwangju Metropolitan Mhe. Lee Jeong ameishukuru Serikali kupitia TET kwa kusimamia vizuri mradi huu na kuhakikisha wanafunzi wananufaika na mradi huo.
Amesema, Gwangju itaendelea kuisaidia Tanzania hasa katika eneo la TEHAMA ili kuongeza kasi ya maendeleo kupitia elimu.
Nae, Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Tegeta A ameshukuru kupatiwa vifaa hivyo huku akitanabaisha vifaa hivyo vimesaidia sana katika kupunguza changamoto ya vitabu kwani sasa vitabu vinapatikana katika maktaba mtandao kupitia vifaa walivyopatiwa.