The House of Favourite Newspapers

Msomi chuo kikuu auawa

0

msomiShelitiael Steven Mbise enzi za uhai wake.

Shani Ramadhani

RIP! Kijana aliyefahamika kwa jina la Shelitiael Steven Mbise, aliyekuwa akisoma Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) amefariki dunia kwa kuchomwa kisu na muuza chipsi kufuatia kutofautiana.

Kwa mujibu wa chanzo kutoka Dodoma, denti huyo alikuwa akichukua masters akiwa kwenye mwaka wake wa kwanza.

“Marehemu alikuwa amepanga chumba nje ya chuo, Mtaa wa Chako ni Chako lakini kipindi hiki chuo kimefungwa alikuwa hapa na mara nyingi alikuwa akionekana yuko bize na masomo kwani alikuwa akienda chuoni na kurudi.

“Kuna sehemu alishawahi kupanga chumba na rafiki yake lakini baadaye akahama na kwenda kupanga chumba chake mwenyewe,” kilieleza chanzo hicho kwa sharti la kutotajwa jina.

Chanzo kiliendelea kuweka wazi kuwa siku ya tukio, Alhamisi ya Septemba 10, mwaka huu Mbise alikwenda kwenye chipsi ambapo ni jirani na anapoishi. Ndipo kukatokea mgogoro ulisababisha muuza chipsi kumchoma kisu.

“Kulikuwa na ugomvi kati ya marehemu na muuza chipsi. Sasa mashuhuda wanadai, msomi huyo aliomba chenji yake baada ya kula, muuza chipsi akasema hajalipa na akamtaka alipe. Wakazozana, mwishowe msomi aliamua kuondoka, ndipo mtu wa chipsi akamfuata kwa nyuma na kumchoma kisu sehemu ya juu ya mgongo. Mbise alianguka na kupoteza maisha palepale huku mtuhumiwa akishikiliwa,” kilisema chanzo.

Kikaendelea: “Baada ya hapo, taarifa ziliufikia uongozi wa chuo na mwili ulichukuliwa na kupelekwa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya uchunguzi na kisha Ijumaa usiku ulisafirishwa kwao jijini Arusha.”

Kupitia simu ya mkononi, mwandishi wetu alimpigia afisa habari wa chuo hicho ambaye alijitambulisha kwa jina moja la Beatrice. Yeye alithibitisha kutokea kwa kifo cha mwanafunzi huyo akisema:

“Ni kweli yule alikuwa mwanafunzi wetu wa mwaka wa kwanza na kipindi hiki chuo kimefungwa lakini yeye alikuwa maeneo ya jirani na chuo kwa ajili ya kuonana na supavaiza wake.

“Siku ya tukio marehemu alikuwa akienda mjini, akapita sehemu wanayouza chipsi kwa ajili ya kupata chakula ndipo ukatokea ugomvi uliosababisha yeye kuchomwa kisu lakini kesi tayari ipo polisi na yule mtuhumiwa anashikiliwa katika Kituo Kikuu cha Polisi Dodoma.

Mwili wa Steven Mbise ulihifadhiwa kaburini Jumamosi iliyopita. Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina.

JIUNGE NA GLOBAL BREAKING NEWS!

Leave A Reply