The House of Favourite Newspapers

Msongamano Waua Watu Sita AFCON Cameroon

0


WATU sita wameripotiwa kufariki na makumi kadhaa kujeruhiwa katika msongamano uliotokea nje ya uwanja unaopokea mechi za Kombe la Mataifa ya Afrika nchini Cameroon.

 

Picha za video zinaonyesha mashabiki waking’ang’ana kuingia kwa nguvu katika uwanja Paul Biya uliopo katika mji mkuu YaoundeNaseri Paul Biya, gavana wa jimbo la kati la Cameroon amesema kuwa huenda kukawa na idadi zaidi ya waathiriwa , limesema Shirika la habari la AP.

 

Ripoti nyingine imesema kuwa watoto kadhaa walikuwa wamepoteza fahamu. Uwanja huo una uwezo wa kuwapokea watu 60,000, lakini kwasababu ya masharti ya kuzuwia maambukizi ya Covid ulipaswa kupokea 80% pekee ya watu hao.

 

Maafisa wa mechi waliripotiwa wakesema kwamba watu wapatao 50,000 walikuwa wakijaribu kuingia ndani ya uwanja huo. Msongamano katika lango la uwanja ulisababisha “vifo vya watu sita na makumi kadhaa wamejeruhiwa”, aliripoti mtangazaji wa kituo cha televisheni cha taifa CRTV.

 

Nick Cavell, mzalishaji wa vipindi wa BBC Afrika, alikuwa katika mechi na anasema kwamba ilionekana taarifa ya mkanyagano haikuwafikia umati wa watu hadi taarifa iliporipotiwa kwenye mitandao ya kijamii. 

 

Viatu vingi na vifusi vilionekana kwenye lango la kuingia uwanjani, alisema. Muuguzi Olinga Prudence aliliambia shirika la habari la AP kwamba baadhi ya majeruhi walikuwa katika “hali mbaya”.

 

Shirikisho la soka barani Afrika, CAF limesema katika taarifa yake kwamba kwa sasa “linachunguza hali na kujaribu kupata taarifa zaidi za kile kilichotokea”.

 

Mechi ya mwisho ya 16 baina ya Cameroon na Comoro, ilichezwa licha ya tukio hilona ilimalizika kwa ushindi wa wenyeji Cameroon wa 2-1 dhidi ya Comoro.

Leave A Reply