The House of Favourite Newspapers

Mstaafu Auawa Kikatili na Mfanyakazi wa Ndani Ili Achukue Mafao

TUNSUME Sakajinga (60), mkazi wa wilayani Mgeninani, Kijichi, Temeke jijini Dar es Salaam ameuawa baada kupigwa na kitu kizito kichwani kisha kuchomwa na mkasi shingoni na mtu anayedaiwa kuwa kijana wake wa kazi za nyumbani.

 

Tukio hilo lilitokea Jumamosi, Januari 12, mwaka huu nyumbani hapo ambapo marehemu alikuwa akiishi na huyo kijana huyo akimsaidia kazi mbalimbali zikiwamo za nyumbani na shambani.

 

Akisimulia mkasa huo, mkwe wa dada wa marehemu ambaye hakutaka kutaja jina lake, jana Jumatatu Januari 14, amesema marehemu alikuwa akiishi peke yake nyumbani kwake hapo na kijana huyo ambaye aliishi nae mwaka 2017 kabla ya kuondoka na kurudi tena Septemba mwaka jana.

 

“Siku ya tukio marehemu alitoka kwenda dukani akarudishia milango, lakini alivyorudi akakuta milango imefungwa hali iliyomshtua kwani yeye hakuacha mtu ndani. Alivyokuta mlango umefungwa akampigia simu fundi anayemjengea na anayemsaidia akiwa na shida mbalimbali, kumuelezea kuna mtu ndani wakati yeye alipotoka hakuacha mtu, hivyo akabaki nje akimsubiri fundi.

 

“Baada ya muda mfupi, fundi alipofika akakuta geti limefungwa akagonga bila mafanikio na akipiga simu hazipatikani akachukua jukumu la kuwaita mafundi wenzie wakashirikiana kugonga lakini ikashindikana ikabidi waende kwa Mwenyekiti wa Mtaa na kisha polisi walipofika eneo la tukio waliruka ukuta na walipoingia ndani wakakuta milango yote imefungwa lakini kupitia dirisha la jikoni waliona kitu kimefunikwa kwa mkeka.

 

“Kwa sababu milango ilikuwa imefungwa walitumia bomba refu kufunulia mkeka huo ambapo walikuta mwili wa marehemu ukiwa na mchi na mkasi uliotumika kumchomea, wakabomoa milango na kuingia ndani.

 

“Walipoingia ndani walikuta mikeka mingine imefunikwa na walipoifunua walimkuta kijana huyo ambaye alianza kupiga kelele na kusema msiniue siyo mimi niliyefanya hivyo bali tulivamiwa na majambazi,” ameeleza.

 

Hata hivyo, mkwe huyo amesema inahisiwa kijana huyo alifanya hivyo ili achukue mafao ya marehemu ambaye mwanzoni alikuwa mfanyakazi wa Mamlaka ya Bandari (TPA), na alistaafu Desemba 30 mwaka jana.

 

Aidha, amesema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Temeke ukisubiri taratibu za kipolisi kabla ya kusafirishwa kwenda kuzikwa Tukuyu jijini Mbeya.

 

Kamanda wa Polisi mkoa wa kipolisi Temeke, Emmanuel Lukula amethibitisha kuwapo kwa tukio hilo lakini amesema bado wanafanya uchunguzi kubaini nani alihusika na kwamba hakuna mwenye uhakika kama aliuawa na mvulana wake wa kazi.

 

“Hilo bado tunachunguza na hakuna mwenye uhakika kama ‘houseboy’ wake ndiye alimuua. Siwezi kuthibitisha ila bado tunachunguza,” amesema.

RC Mwanri Ashtuka Aagiza Uchunguzi wa Mradi wa Maji

Comments are closed.