The House of Favourite Newspapers

Msuva: Simba wakitulia, Al Ahly anakufa Taifa

WINGA wa zamani wa Yanga ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa Morocco, Saimon Msuva, amewataka wachezaji na benchi la ufundi la Simba kutulia ili wafanye kweli kwenye mechi yao ya marudiano mbele ya Waarabu wa Misri, Al Ahly.

 

Simba inayoshiriki Ligi ya Mabingwa Afrika Hatua ya Makundi, wikiendi iliyopita ilijikuta ikifanywa vibaya na Al Ahly baada ya kufungwa mabao 5-0. Mechi hii ilipigwa kwenye Uwanja wa Borg El Arab nchini Misri.

 

Timu hizo zitarudiana tena jijini Dar es Salaam Februari 12, mwaka huu ambapo safari hii Simba watakuwa wenyeji wa Waarabu hao ambao ni vinara katika kundi D wakiwa na pointi saba, Simba wenyewe wana pointi tatu.

 

Msuva ambaye anaichezea Difaa El Jadida, ameliambia Championi Jumatano, kuwa Simba wanatakiwa watulie kuhakikisha kwamba wanapata matokeo mazuri kwenye mechi hiyo dhidi ya Al Ahly sambamba na mechi zake nyingine mbili ambazo wamezibakisha hatua ya makundi.

 

“Simba ni timu nzuri na wamesajili wachezaji wazuri, hatua hii waliopo wao mimi nilicheza nikiwa na Yanga lakini pia nilishiriki nikiwa Jadida mwaka jana ila tukaishia hatua hii ya makundi. “Kikubwa ninachowaambia ni kwamba wasikate tamaa kwa matokeo wanayoyapata, kiukweli ni matokeo mabaya, hakuna mtu anayefurahia hayo matokeo kwa sababu wao wapo kama nchi, wanacheza kama nchi na siyo Simba.

 

“Kwa upande wangu ninasema wanatakiwa wapambane kwenye mechi zilizobakia watakazocheza nyumbani wapate matokeo, hicho ndiyo kikubwa na tuwape sapoti, wakifanya vizuri wanatupa sifa taifa zima. “Wakijituma na kupambana kwenye michezo yao ijayo ukiwemo ule dhidi ya Al Ahily, na wakitambua kuwa wao ni bora basi watakuwa na nafasi kubwa ya kupata ushindi,” alisema Msuva.

JIUNGE NA FAMILIA YA GLOBAL TV UPANDE MTANDAO WA MAFANIKIO

Bofya hapa kujiunga na familia ya Global TV Club ==> Global TV Family Club

Comments are closed.