Kukosekana Kwa Intaneti Shida Ni Mkongo Wa Baharini
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mhe. Nape Moses Nnauye (Mb) amesema kukosekana kwa huduma ya Mtandao wa Intaneti nchini tarehe 12 Mei, 2024 kumetokana na hitilafu kwenye nyaya za baharini (Mkongo wa Baharini) zinazosambaza huduma ya intaneti na simu za kimataifa.
Waziri Nape ametoa taarifa hiyo kupitia ukurasa wake wa X (Twitter) na kubainisha kuwa juhudi za kutatua tatizo hilo zinaendelea.
Amesema taarifa ya awali iliyotolewa kutoka kwa watoa huduma wa nyaya za baharini, kama vile Seacom na EASSy, inaonyesha kuwa lipo tatizo kwenye nyaya hizo zilizoko kati ya Msumbiji na Afrika Kusini.
“Wakati wa mchakato wa marekebisho, upatikanaji wa huduma za intaneti na simu za kimataifa utakuwa wa kiwango cha chini, na watumiaji watalazimika kutumia njia mbadala hadi tatizo hili litakapotatuliwa,” ameeleza Waziri Nape.
Waziri Nape amewaomba radhi watumiaji wa huduma za Intaneti nchini kwa usumbufu wowote uliotokana na tatizo hilo.