The House of Favourite Newspapers

Mtanzania Atunukiwa Ushindi wa Mr Albino Afrika Mashariki 2018

Emmanuel Silas Shedrack (aliyekaa kushoto) mshindi wa Mr Albino akiwa na Maryanne Muigai aliyetawazwa kuwa Miss Albino katika mchuano wa Mr and Miss Albinism East Africa 2018 jijini Nairobi, Kenya, Ijumaa iliyopita.

MTANZANIA Emmanuel Silas Shedrack (20) ametawazwa Mr Albino katika mashindano ya uzuri na mvuto yaliyoshirikisha maalbino wanawake na wanaume kutoka nchi za Kenya, Uganda na Tanzania.

Mashindano hayo yalitayarishwa na  Chama cha Maalbino cha Kenya (Albinism Society of Kenya) na kuzishirikisha nchi hizo tatu za Afrika Mashariki katika mchuano wa  Mr and Miss Albinism East Africa 2018 uliofanyika jijini Nairobi Ijumaa iliyopita.

Mashindano hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Kenyatta International Convention Centre (KICC) na kujumuisha washindani 30, yalilenga kuwaonyesha walimwengu kwamba maalbino wanapendeza na kuvutia kama watu wengine licha ya mwonekano wa ngozi zao.

Washindi hao wawili, watazawadiwa fedha taslimu na watakuwa mabalozi wa jumuia mbalimbali zinazohusiana na chama chao.

Mmoja wa washiriki wa mchuano huo ambaye ni Mtanzania, Elizabeth James, akihojiwa kwenye tukio hilo alisema alipokuwa mtoto ilibidi ahame shule kila mara baada ya kugundua kwamba kulikuwa na watu wanamwonyesha vidole na kumfuata sehemu mbalimbali kila mara wakiwa na nia mbaya.

Alitoa wito kwa watu kuacha imani za kipuuzi zinazosababisha kuuawa kwa maalbino ili kupata sehemu za viungo vyao au kufukua makaburi yao wakitafuta viungo hivyo kwa imani ya kupata utajiri au bahati nzuri.

“Hata hivyo, tishio hilo limepungua sana, lakini bado lipo, alisema.

Comments are closed.