The House of Favourite Newspapers

Mtoto alivyoliwa na mbwa

0


Marehemu Jovina Rwegasira Enzi za uhai wake
Mtoto Jovina  Rwegasira, aliyeumwa na mbwa.

Johnson James na Idd Mumba

Mtoto mmoja mkazi wa Malimbe jijini Mwanza aliyefahamika kwa jina la Jovina  Rwegasira, 7, (pichani) aliyekuwa akisoma kwenye Kituo cha Chekechea cha ABC Malimbe, amefariki dunia baada ya kuvamiwa na mbwa 12 kisha kung’atwa hadi kufa baada ya kunyofolewa sehemu mbalimbali za mwili wake.

mama mzazi wa Jovina Rwegasira, Chausiku HarunaMama mzazi wa Jovina Rwegasira, Chausiku Haruna

Akizungumza na gazeti hili mama mzazi wa mtoto huyo, Chausiku Haruna alisema mtoto wake aling’atwa na mbwa hao baada ya kutumwa na msichana wa kazi kwenda dukani kununua mafuta ya kupikia Septemba 18, mwaka huu.

“Wakati tukio linatokea mimi nilikuwa kazini kwani kazi yangu ni kuwapikia chakula mafundi ujenzi, sasa siku hiyo hawakuwepo ikabidi nirudi nyumbani.

“Nilipofika maeneo ya Vanesa karibu na nyumbani kwangu niliona watu wamejazana huku wakishangaa, baada ya kufika nikaambiwa mwanangu ameliwa na mbwa mpaka amefariki dunia, nikahisi kuchanganyikiwa ikabidi nisogee nikaone, nikakuta kweli mwanangu amefariki dunia,” alisema mama huyo.

Aliongeza kuwa ilibidi polisi waitwe, walipofika waliuchukua mwili wa mwanangu na kuupeleka hospitali kwa uchunguzi.

“Marehemu alifikishwa kwenye Kituo cha Afya cha Igogo kilichopo wilayani Nyamagana na madaktari walithibitisha alikwisha fariki dunia ndipo ukapelekwa kuhifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando,” alisema.

Majirani walisema kwamba mbwa hao waliomuua mtoto huyo wanaishi kwenye msitu ambao uko karibu na Chuo cha Sauti Malimbe jijini hapa na hawana mwenyewe kutokana na chuo kufungwa, hawapati chakula hivyo kumtafuna mtoto huyo.

Baada ya tukio hilo, wananchi waliingia katika msituni huo na kuwasaka wanyama hao ambapo walifanikiwa kuwaua zaidi ya mbwa 60.

Leave A Reply