HURUMA kwa mtoto huyu! Ndivyo unavyotakiwa kusema kutokana na bibi mmoja aliyejitambulisha kwa jina la Sada William, kujikuta katika wakati mgumu baada ya mjukuu wake, Mayra Ajmerry (10) kuugua ugonjwa wa mapafu na moyo kuwa na tundu na kumsababishia kushindwa kupumua, hivyo kudaiwa gharama za matibabu ya shilingi milioni 80 nchini Kenya.
Akizungumza kwa uchungu na UWAZI kuhusu afya ya mjukuu wake, bibi wa mtoto huyo alisema, binti yake alipojifungua mtoto Mayra katika Hospitali ya Mount Meru Arusha, walihisi ana matatizo ya upumuaji, lakini baada ya kuuliza kwa madaktari, wakaambiwa kuwa yupo sawa, lakini waliporudi nyumbani baada ya siku saba, hali yake ilibadilika na kuwa mbaya.
Akaendelea kusimulia: “Ikabidi turudi tena hospitali, tukapewa jibu lilelile na madaktari kuwa, mtoto yupo sawa. Tukaamua kumpeleka Hospitali ya Seliani, Arusha.
“Tulipofika akawekwa kwenye chumba cha joto cha watoto njiti, alikaa pale miezi mitatu, baadaye madaktari wakatuambia turudi nyumbani na wataendelea na uchunguzi ili kujua tatizo ni nini, kwa sababu walisema kuna vipimo vingine hawawezi kumfanyia kwa kuwa ni mdogo sana, hivyo wanasubiri angalau afikishe mwaka mmoja waangalie namna ya kumsaidia.
“Lakini tatizo likawa linaendelea na mtoto akawa anateseka na kupumua kwa shida, ikabidi twende Hospitali ya AICC kwa ajili ya kumcheki kama anatatizo la moyo. Alipopimwa, madaktari wakatuambia mtoto anatundu kwenye moyo na mapafu yana ukungu, akalazwa.
“Baada ya matibabu kwa miezi kumi, hali iliendelea kuwa mbaya, madaktari wakatushauri twende nje ya nchi ili akapatiwe matibabu zaidi.
“Tukaondoka kuelekea Hospitali ya Gertude’s Childrens iliyopo jijini Nairobi, Kenya. Wakampima na kuona kweli ana ukungu kwenye mapafu, wakamuwekea mipira ili kuuondoa ukungu, kisha akawekwa kwenye chumba cha wagonjwa wenye uangalizi maalum (ICU), ambapo alikaa kwa siku tatu, ya nne akafanyiwa upasuaji wa kuziba tundu kwenye moyo.
“Madaktari wametwambia kuwa, uwezekano wa mtoto kupona upo, lakini itachukua muda mrefu, na tunatakiwa kulipia gharama za matibabu shilingi milioni 80. Tumejitahidi tumepata shilingi milioni 50, bado shilingi milioni 33.
“Tunawaomba Watanzania walioguswa na tatizo hili, watuchangie kiasi chochote kupitia simu yangu mimi bibi yake, kwa namba 0763 272 443 jina Sada William Mhoe, au kupitia benki akaunti namba; NMB Acc No.40810082837- Costence Benjamin Mgalu,” alisema Sada.
HABARI; Memorise Richard , Uwazi