The House of Favourite Newspapers

Mtoto wa Mondi Ampa Utajiri Tanasha, Akaunti Yasoma Bil 3

0

RIPOTI za mastaa walioingiza pesa ndefu kwa mwaka huu wa 2020, zimeanza kutoka ambapo kitendo cha msanii wa muziki wa Kenya, mwanamama Tanasha Donna Oketch kuzaa na staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, kinatajwa kumpa utajiri mkubwa.

 

SHUKURANI KWA NASEEB JUNIOR

Utajiri wa Tanasha unaelezwa kuwa, ameupata baada ya kuwa kwenye uhusiano na Diamond au Mondi, hivyo shukurani zimuendee mtoto aliyezaa naye aitwaye Naseeb Junior.

Imeelezwa kwamba, mtoto huyo wa Mondi, amempa Tanasha umaarufu na kujikuta akifanya vizuri kupitia muziki wake, ambao sasa unafuatiliwa, kutazamwa, kuuza zaidi na kumuingizia mkwanja mrefu.

 

DOLA MIL 1.5

Ukiachilia mbali malalamiko ya Tanasha kwamba, Mondi hamsaidii kumlea mtoto wao huyo, lakini utajiri wake unakadiriwa kufikia Dola za Kimarekani milioni 1.5 (zaidi ya shilingi bilioni 3 za Kitanzania) hadi kufikia Agosti, mwaka huu.

ALIANZA KWENYE UREMBO

Mbali na muziki, kama mwanamke mfanyabiashara, Tanasha alianza kwa kuwekeza kwa ukubwa kwenye tasnia ya urembo, akijihusisha na biashara ya vipodozi na nywele za wanawake, eneo ambalo ndilo lilikuwa fani yake kabla ya kujikita kwenye utangazaji na muziki.

 

Tanasha anamiliki kampuni kubwa ya bidhaa za urembo ya For Her Luxury Hair, ambayo ni msambazaji mkubwa wa nywele za bei mbaya za wanawake za kutoka ughaibuni katika nchi za Afrika Mashariki.

Mbali na hivyo, pia Tanasha ana madili kibao ya ubalozi wa bidhaa (brand ambassador) akiwa na wafuasi zaidi ya milioni 2.5 kwenye ukurasa wake wa Instagram.

MUZIKI UNAVYOMTOA

Kwa mujibu wa Kampuni ya Popnable ambayo hudili na kutathmini mafanikio ya kipesa ya wasanii nchini Kenya, Tanasha alijiingiza kwenye muziki tangu mwezi Mei, mwaka jana, mara tu baada ya kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na Mondi.

 

Tangu hapo, muziki wa Tanasha umekuwa ukiuza zaidi kwenye mitandao (platforms) mbalimbali za muziki kama Slacker Radio, Vevo, Audiomack, YouTube, Mdundo, Deezer, TuneIn, Tidal, 8tracks, Mixcloud, iHeartRadio, MySpace, SoundCloud, Xbox, Pandora, Google Play, Spotify, Vimeo, iTunes, Boomplay na nyinginezo.

 

NYIMBO ZILIZOUZA ZAIDI

Baadhi ya nyimbo za Tanasha zilizofanya vizuri zaidi kwenye mauzo kwenye mitandao hiyo, ni pamoja na La Vie, Gere, Liar, Ride, Nah Easy, Sawa, Jacuzzi, Te Amo, Radio na nyingizo kutoka kwenye EP yake ya Donnatella.

REKODI ZA MKWANJA MWAKA 2019

Zifuatazo ni rekodi za mkwanja alioingizia Tanasha kwenye mabano tangu mwezi Mei, mwaka jana hadi Agosti mwaka huu;

Mei, 2019 (Dola za Kimarekani 1,900), Juni (Dola za Kimarekani 1,480), Julai (Dola za Kimarekani 1,300), Agosti (Dola za Kimarekani 1,460), Septemba (Dola za Kimarekani 750), Oktoba (Dola za Kimarekani 790), Novemba (Dola za Kimarekani 1,140) na Desemba (Dola za Kimarekani 900).

 

MWAKA 2020

Mwaka 2020 mambo hayakuwa mabaya, ambapo ripoti za kiasi cha pesa alizoingiza, zinasomeka hivi;

Januari (Dola za Kimarekani 4,000), Februari (Dola za Kimarekani 2,400), Machi (Dola za Kimarekani 4,500), Aprili (Dola za Kimarekani 6,900), Mei (Dola za Kimarekani 1,800), Juni (Dola za Kimarekani 3,400), Julai (Dola za Kimarekani 717) na Agosti (Dola za Kimarekani 2,900).

SHOO VIPI?

Kuhusu shoo alizofanya na kuingiza pesa ndefu, Tanasha anasema; “Naweza kusema shoo bado, hazikuwa kwa ukubwa kwa sababu ya COVID-19 (Virusi vya Corona).”

 

MJENGO WA KIFAHARI

Mara tu baada ya kutengana na Mondi mapema mwaka huu, Tanasha alitangaza kununua mjengo wa kifahari jijini Nairobi na kuhamia kwenye nyumba hiyo akiwa na mwanaye huyo.

 

Tanasha alisema kuwa, nyumba hiyo alinunua kwa nguvu zake mwenyewe kutokana na kazi zake na kisanaa na wala hakukuwa na mkono wa mwanaume yeyote.

MAGARI MAKALI

Ukiacha lile gari la kifahari aina ya Toyota Land Cruiser Prado V8 alilopewa na Mondi wakati wa sherehe ya siku yake ya kuzaliwa pale Mlimani City jijini Dar na kuliacha aliporudi kwao, kabla ya hapo Tanasha alikuwa tayari anamiliki gari kali aina ya Mercedes Benz lenye rangi ya bluu.

 

Hivi karibuni, pia Tanasha alidai kujizawadia nyumba nyingine na gari lingine jipya aina ya Mercedes Benz lenye rangi nyeupe, alipokuwa akisherehekea siku yake ya kuzaliwa Julai 7, mwaka huu wakati akitimiza umri wa miaka 25.

 

TANASHA: MENGI YANAKUJA

Kwa mujibu wa Tanasha, bado ana mengi jikoni ambayo anayapika na atayapakua hivi karibuni. Kwa sasa Tanasha anajivunia kuwa kwenye kilele cha mafanikio yake.

 

Hata hivyo, pamoja na kujimwambafai kwake, lakini kwa mujibu wa wachambuzi wa habari za burudani Afrika Mashariki, Tanasha amefikia kwenye mafanikio hayo kutokana na kitendo cha kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi na kuzaa na Mondi, ambacho kilimpaisha mno na kumfungulia milango ya utajiri huo.

TUJIKUMBUSHE

Tanasha alirejea nyumbani kwao nchini Kenya mnamo Februari, mwaka huu baada ya kutengana na Mondi. Wakati wanaachana, wawili hao walikuwa wameachia wimbo wa pamoja wa Gere ambao ulikuwa ukivuma mno, jambo ambalo baadhi ya mashabiki waliamini ni kiki, lakini baadaye ilibainika kwamba, ilikuwa ni kweli wametengana jumlajumla.

STORI: SIFAEL PAUL, RISASI JUMAMOSI 

Leave A Reply