
Kesi ya mauaji inayomkabili Timothy Gitonga mwenye umri wa miaka 30, anayetuhumiwa kumuua bibi yake, Journes Kiringa mwenye umri wa miaka 80, imeshindwa kusikilizwa kufuatia mtuhumiwa huyo kuzidiwa na maradhi akiwa kizimbani.
Kesi hiyo ilikuwa ikisikilizwa katika Mahakama ya Embu, nchini Kenya ambapo mtuhumiwa alipoingizwa mahakamani, alianza kulalamikia maumivu makali aliyokuwa akiyahisi, jaji akaamuru kesi iendelee lakini mtuhumiwa aliendelea kulalamikia maumivu makali huku akionesha kuzidiwa.
Kufuatia hali hiyo, Jaji Tony Kwambai aliamua kusitisha usikilizwaji wa kesi hiyo na kuagiza mtuhumiwa apelekwe katika Hospitali ya Embu na baada ya matibabu arejeshwe katika Kituo cha Polisi Itabua kisha apelekwe tena mahakamani hapo ifikapo Januari 17, mwaka huu.
Mtuhumiwa huyo alikamatwa baada ya kudaiwa kumshambulia bibi yake na kumuua huku akimjeruhi vibaya babu yake, Jamleck Wamai ambaye anaendelea na matibabu katika Hospitali ya Embu.
Tukio hilo lilitokea katika Kijiji cha Rungana, Nembure ambapo sababu za tukio hilo hazijafahamika na baada ya kutenda ukatili huo, mtuhumiwa alitoroka kabla ya kukamatwa na polisi.

