HATIMAYE baada ya kiungo wa Yanga, Tonombe Mukoko kuhusishwa kuhitajika na miamba ya soka kutoka Afrika Kusini, Kaizer Chiefs, kiungo huyo ameweka wazi ishu hiyo huku yeye mwenyewe akisema kuwa taarifa hizo anazisikia kama tetesi.
Mukoko aliliambia Championi Jumamosi kuwa, yeye kama mchezaji amekuwa akisikia tetesi mbalimbali kuhusu kutakiwa na Kaizer Chiefs lakini yeye hajui lolote kwani kama ikitokea anatakiwa kuuzwa basi Yanga ndio wanahusika kwa kuwa yeye bado ana mkataba na Wanajangwani hao.
“Kuhusu kuhitajika na Kaizer Chiefs, nimesikia taarifa hizo, lakini kwangu sifahamu lolote kabisa kwani kila kitu kuhusu mimi kipo katika mikono ya Yanga, kwa kuwa bado nina mkataba nao.
“Hivyo ikitokea nimeuzwa basi fahamu Yanga ndio watakuwa wameniuza, bado mimi ni mchezaji wa Yanga na nitaendelea kuwa hapa, kwa sasa ninaangalia namna gani pamoja na wachezaji wenzangu tunapambana kwa ajili ya kuipatia mafanikio timu, ikiwemo kutwaa ubingwa,” alisema mchezaji huyo.
Tonombe alirejea nchini juzi usiku na kujiunga kambi ya Yanga iliyoweka Kijiji cha Avic Town, Kigamboni nje ya Jiji la Dar es Salaam akitokea kwenye majukumu ya timu ya Taifa ya DR Congo iliyocheza michezo miwili dhidi ya Gabon na Gambia.
STORI: MARCO MZUMBE NA HUSSEIN MSOLEKA