The House of Favourite Newspapers

Mukoko Aipiga Mkwara Simba

0

KUELEKEA mchezo wa Ngao ya Jamii dhidi ya wapinzani wao wa jadi klabu ya Simba Jumamosi hii, kiungo mkabaji wa Yanga, Mukoko Tonombe ameweka wazi kuwa anaamini kikosi chao kina nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi katika mchezo huo.

 

Simba na Yanga zitakutana Jumamosi ya wiki hii katika mchezo wa Ngao ya Jamii unaotarajiwa kuchezwa kwenye Uwanja wa Mkapa Dar es Salaam, ambapo Mukoko anatarajiwa kuukosa mchezo huo kutokana na kadi nyekundu aliyoipata kwenye mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam Julai 25, mwaka huu.

 

Mara ya mwisho kwa klabu hizo kukutana ilikuwa Julai 25, mwaka huu katika mchezo wa fainali ya Kombe la Shirikisho (FA), ambapo Simba waliibuka na ushindi wa bao 1-0 na kutetea taji hilo ambalo walilitwaa msimu wa 2019/20.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mukoko alisema: “Tumefanya usajili bora msimu huu na licha ya kwamba hatujawa na mwanzo mzuri katika michezo yetu miwili ya kwanza mbele ya mashabiki wetu, lakini bado tuna imani kubwa na timu yetu na mipango ambayo tunayo kwa msimu ujao.

 

“Tutacheza dhidi ya Simba Septemba 25, ni mchezo mgumu lakini kama kikosi tumejipanga vizuri na naamini kuwa tutaibuka na ushindi katika mchezo huo,” alisema kiungo huyo.

JOEL THOMAS, Dar es Salaam

Leave A Reply