Mvua Yaezua Paa Sekondari Bukoba, Shule Yafungwa
MVUA kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia leo ikiambatana na upepo mkali, imesababisha madhara makubwa katika Shule ya Sekondari ya Bukoba ambayo imefungwa na wanafunzi zaidi ya 800 kuhamishiwa katika shule za sekondari za Ihungo na Omumwani.
“Wanafunzi wote mnaosoma katika shule hii kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne mtahamia katika shule ya sekondari ya Ihungo na wanafunzi wa kidato cha tano na sita mtahamia shule ya sekondari ya Omumwani,” amesema Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, Deodatus Kinawiro, baada ya kuifunga Shule ya Sekondari ya Bukoba.
Inaelezwa kwamba pamoja na uharibifu huo, shule hiyo haikuwa katika hali nzuri kutokana na baadhi ya majengo yake kuathirika na janga la tetemeko la ardhi lililoikumba Kagera, Septemba 10, 2016.
Aidha, inasemekana baadhi ya vyumba vimefungwa kutokana na kutofanyiwa ukarabati jambo linalochangia mlundikano wa wanafunzi madarasani. Hata hivyo, bodi ya shule hiyo iliiomba serikali kuifunga haraka shule hiyo na kuyakarabati majengo yake yanayohatarisha usalama wa wanafunzi kutokana na kuchakaa.
Comments are closed.