The House of Favourite Newspapers

Mwakifwamba Afungukia Ishu ya Wasanii na Kampeni za 2015, Asema Shirikisho la Filamu TZ Halijasajiliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa

RAIS wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Simon Mwakifwamba amesema kuwa mikataba na makubaliano ya kuwapigia debe wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015 hayakuhusisha shirikisho hilo na yeye kama rais wa shirikisho hana taarifa hizo.

Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), Simon Mwakifwamba akizungumza na wanahabari leo.

“Ninachokifahamu ni kwamba, kila msanii alikuwa na mkataba wake binafsi hivyo shirikisho lisingeweza kumzuia msanii kujihusisha na masuala ya kisiasa kwa chama anachokitaka.

“Hata hivyo, Shirikisho la Filamu Tanzania si kwamba limesajiliwa na Msajili wa Vyama vya Siasa, la hasha! Lipo chini ya Usajili wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA).” Alisema Mwakifwamba.

Mwakifwamba ametoa rai kwa mtu anayesambaza taarifa za uchochezi juu yake kuhusiana na mkutano na wanahabari uliodaiwa kuwa ungefanyika Jumapili, atachukuliwa hatua kali za kisheria mara utaratibu kutoka mamlaka zinazohusika na masuala ya mitandao utakapokamilika.

Alisema kuwa ujumbe uliosambazwa ulisema kuwa siku hiyo angelizungumzia wasanii jinsi walivyolipwa fedha za kupiga kampeni wakati wa uchaguzi na mambo yanayoendelea juu ya wasanii wanaosambaziana maneno mitandaoni.

NA DENIS MTIMA | GLOBAL PUBLISHERS

Comments are closed.