The House of Favourite Newspapers

Mwambusi Ashtuka, Amsuka Yacouba

0

BAADA ya kuanza na sare ya bao 1-1, Kocha Mkuu wa Yanga, Juma Mwambusi, amesema kuwa amegundua tatizo katika kikosi chake ambalo amepanga kulifanyia kazi haraka ili kuhakikisha anapata matokeo mazuri ya ushindi.

Yanga juzi kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam walicheza dhidi ya KMC FC na kutoka sare ya bao 1-1.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mwambusi alisema kuwa tatizo lililosababisha timu yake ishindwe kupata matokeo mazuri ya ushindi dhidi ya KMC ni umakini mdogo wa safu yake ya ushambuliaji inayoongozwa na Warundi Said Ntibazokinza ‘Saido’, Fiston Abdolurazack na Muivory Coast, Yacouba Sogne.

 

Mwambusi alisema kuwa amepanga kulifanyia kazi tatizo hilo la ushambuliaji kwa haraka ili kuhakikisha wanazitumia vema nafasi ambazo timu hiyo inazipata katika ligi na Kombe la FA.

 

Kocha huyo alisema kuwa kama safu yake ya ushambuliaji ingekuwa makini, basi timu hiyo isingemaliza kwa matokeo hayo ya sare na badala yake kupata ushindi kutokana na nafasi ambazo wamezipata.

 

Aliongeza kwa kuwataka mashabiki wa timu hiyo kuungana kwa pamoja na kuwapa morali wachezaji wao baada ya sare hiyo ili katika michezo ijayo ya ligi na FA wafanye vizuri.

“Matokeo ya sare tuliyopata dhidi ya KMC siyo mabaya sana na kikubwa mashabiki wanatakiwa kuungana kwa kuwasapoti wachezaji wetu katika kuwaongezea morali na hali ya kujituma.

 

“Bado timu yetu ina nafasi ya kupata matokeo mazuri ya ushindi na hilo linawezekana kwetu, katika mchezo wetu dhidi ya KMC tulitakiwa kupata ushindi kutokana na nafasi ambazo tumezipata za kufunga.

 

“Nimeliona tatizo hilo la ushambuliaji hivyo nimepanga kulifanyia kazi ili kuhakikisha tunatumia kila nafasi tutakayokuwa tunaipata kama ilivyokuwa tulivyocheza dhidi ya KMC, tulipata nafasi nyingi lakini tukashindwa kuzitumia,” alisema Mwambusi.

STORI NA WILBERT MOLANDI | CHAMPIONI JUMATATU

Leave A Reply