The House of Favourite Newspapers

Mwanamke ammwagia mwanaume maji ya moto

0

IMG_2252
Abdallah Adamu akipata tabu ya kukaa kutokana na jeraha alilolipata baada ya kumwagiwa maji ya moto.

Stori: Mayasa Mariwata na Makongoro Oging’
Huu ni ukatili ulioje! Mwanamke aliyetajwa kwa jina la Eva Mwakajinga (32), mkazi wa Buguruni jijini Dar, anadaiwa kummwagia maji ya moto na kumuunguza vibaya mgongoni kijana, Abdallah Adamu (21), naye mkazi wa Buguruni kisa kikiwa kinashangaza.

Akizungumza na Ijumaa Wikienda kwa tabu, Abdallah alisimulia kwamba, mwishoni mwa wiki iliyopita, akiwa nje ya nyumba anayoishi akifanya shughuli ndogondogo za nyumbani, alimuona Eva ambaye ni mpangaji mwenzake, akimwaga takataka kwenye eneo lake (Abdallah) baada ya kufanya usafi ndani kwake hivyo kumtaka aziondoe.

IMG_2255“Nilimuona Eva akimwaga uchafu pale nje, nikamwambia autoe kwa sababu ‘site’ (Mamlaka ya Jiji la Dar) siku si nyingi walipita wakawatoza faini watu wanaoharibu mazingira, lakini mwenzangu hakunisikiliza, akaanza kufoka na kudai atakachonifanyia sitasahau maisha yangu yote, wakati hatukuwahi kuwa na ugomvi.

“Sikujua kama anachoongea anamaanisha kwa kuwa sikuona kosa langu, nikamwambia asipoutoa ule uchafu, nitauchukua na kuurudisha ndani kwake ili kuepuka kulipishwa faini, nikaona mwenzangu anaingia ndani.

IMG_2256Muonekano wa jeraha hilo.

“Baada ya muda, nikiwa nimempa mgongo, nilishtuka ananimwagia maji ya moto aliyokuwa akichemsha kunde,” alisema Abdallah akiwa katika hali mbaya nyumbani hapo.

Baada ya kufanya tukio hilo, Eva alikimbilia ndani kisha akajifungia ndipo majirani wakafika na kufanya jitihada za kuvunja mlango kwa kuwa hakutaka kuufungua, wakamchukua na kumpeleka ofisi za kata kisha Kituo cha Polisi cha Buguruni.

Akizungumzia tukio hilo kwa majonzi, mama mzazi wa Abdallah, Ashura Fundi alisema kuwa kitendo alichofanyiwa mwanaye ni cha ukatili uliopitiliza kutoka kwa jirani yao huyo ambaye tangu apange maeneo hayo ana miezi mitatu tu, lakini anaamini sheria itafuata mkondo wake.

“Nilihisi naota, nikajikuta naangua kilio kama mtoto mdogo ila nilikaza moyo tukamkimbiza mwanetu Hospitali ya Kwa-Mnyamani na kuambiwa twende Hospitali ya Amana ambapo alipatiwa matibabu japokuwa hakulazwa kutokana na mazingira ya pale hospitalini.

IMG_2259Akiandaliwa mahali pa kujipumzisha.

“Lakini tunampeleka hospitalini kusafisha kidonda,” alisema mzazi huyo na kuongeza:
“Kutokana na tukio hilo la aina yake lililogubikwa na roho ya ukatili na unyama uliokithiri, Eva bado anashikiliwa kituoni hapo kwa jalada la kesi namba BUG/RB/1218/2016 SHAMBULIO LA KUDHURU MWILI.

Gazeti hili lilifika kituoni hapo na kukutana na polisi aliyekuwa zamu ambaye alithibitisha kushikiliwa kwa Eva na kwamba uchunguzi unaendelea.

Leave A Reply