The House of Favourite Newspapers

Mwinyi Zahera Afanya Mambo 10 Yanga, Yapo Hapa

KUNA mambo 10 ambayo Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera amefanya mpaka mashabiki wanashangaa. Hebu angalia mambo ambayo Kocha huyo mwenye uraia wa DR Congo na Ufaransa amefanya;

KUTOPOTEZA MCHEZO

Yanga ya Zahera imeche­za michezo 14 kwenye ligi kuu mpaka sasa ambapo wameshinda michezo 12 na kutoa sare michezo 2. Ni re­kodi nzuri kwa aina ya kikosi Yanga ilichonacho.

Wamekusanya pointi 38 kwa sasa wana mabao 27 na ni vinara wa kupachika ma­bao wakiongozwa na Heritier Makambo mwenye mabao 7.

Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera.

KUBADILI MATOKEO

Amekuwa na bahati sana kwenye eneo hili. Ni mtu wa mipango mingi hasa ya kutaka kufunga bao la mapema ili awaweke sawa wachezaji wake na kama ikitokea wameanza kufungwa bado ame­kuwa na mbinu muafaka za kuwarudisha mchezo­ni.

Alifanya hivyo katika mchezo dhidi ya Ndan­da ambapo walifungwa mapema baadae wakap­ata faulo wakasawazisha na kutoa sare, pia katika mchezo dhidi ya Mwadui baada ya kusawazishiwa bao kipindi cha pili al­imtoa Klaus Kindoki na kumpa nafasi Ramad­hani Kabwili, akafanikiwa kushinda kwa mabao 2-1.

Kwenye mechi na Pris­ons mambo yalikuwa magumu hasa kutokana na mchezo kuwa na tafra­ni nyingi mpaka dakika ya 70 walikuwa nyuma kwa bao 1 ndipo alipoamua kufanya mabadiliko kwa kumtoa beki Juma Abdul nafasi yake ikachukuliwa na Amissi Tambwe am­baye alibadili matokeo kwa kusababisha penati na kufunga mabao 2.

KUMUAMINI MCHEZAJI

Ni ngumu sana kuwaamini­sha mashabiki wa Yanga kwamba Pappy Tshishimbi anarukaruka tu uwanjani waka­ti wao wanaamini kwamba ndio jembe. Lakini Zahera ame­waambia ukweli. Tshishimbi siyo staa tena Yanga.

Zahera hatazami jina la mchezaji anaangalia juhudi na uwezo wa mchezaji. Juma Abdul alipoumia alimuanzisha Paul Godfrey ambaye ni kinda aliye­washangaza mashabiki kwenye mechi ya Simba na Yanga.

Mchezaji mwingine ni Mo­hammed Jaffary ambaye yupo kikosi cha vijana naye ame­kuwa akimpa nafasi ya kucheza bila kuangalia ni nani atakuwa benchi. Akimuamini mtu haan­galii pembeni.

Ramadhani Kabwili ame­chukua nafasi ya Beno Ka­kolanya ambaye alikuwa go­likipa namba moja kutokana na kile alichoeleza kuwa ni kudai stahiki zake na Klaus Kindoki amekuwa benchi. Mashabiki wanamkejeli Kindoki lakini yeye anaamini bado ana kitu cha kui­fanyia Yanga, hajaja bure.


KUSHINDA MIKOANI

Baada ya kuweza kufani­kiwa kucheza michezo 11 jijini Dar es Salaam wengi walifikiria kwamba itakuwa ngumu kwake kupata matokeo nje ya Dar kutokana na ubovu wa viwanja.

Kashinda mechi zake zote tatu alizocheza nje ya Dar kwa ushindi wa mabao zaidi ya 2 am­bapo mechi yake dhidi ya Prisons ilivuna jumla ya mabao 3-1.

MAAMUZI MAGU­MU

Amekuwa ni mwepe­si kufanya maamuzi ambayo wengi wame­kuwa wakiyashangaa na amekuwa akiyasi­mamia mpaka apate matokeo.

Kwa mfano kiungo mshambuliaji Ibrahim Ajibu ambaye ame­kuwa ni msaada ndani ya timu aliposhindwa kuhudhuria mazoezi muda ambao haku­wepo hakumjumui­sha kwenye kikosi kilichocheza dhidi ya Mwadui na akapata ma­tokeo bila ya kuwa na wachezaji wake kama Kelvin Yondani na Beno Kakolanya. Inahitaji ujasiri kufanya uamuzi kama huu haswa kwa kocha Mwafrika.

MSEMA UKWELI

Viongozi wamekuwa wakificha matatizo yaliyoko ndani ya Yanga lakini yeye wala haogopi anafun­guka tu akiamini kwamba ndiyo njia sahihi ya kupata suluhisho na mashabiki wajue kinachoen­delea.

Kwa sasa msisitizo wake ni kwamba hawezi kufanya usajili wa wachezaji wapya kwa muda huu kwa kuwa kuna wachezaji zaidi ya 10 ambao wamemfuata na kumueleza kuwa hawajalipwa stahiki zao hali ambayo inam­fanya ashindwe kuruhusu kusajili wachezaji wengine.

Pointi yake ya msingi ni kwamba wachezaji hao wapya atakaozungumza nao atawaam­bia nini, hata akiwasajili atawapa nini ilihali wapo ambao wapo ndani ya timu wanadai stahiki zao? Jambo hili linamfanya azidi kuwa tofauti na makocha wen­gine kwa kuzungumza masuala yanayohusu uongozi ili kuweka usawa.

ANAWAPONDA WACHEZAJI

Ni mara chache sana kwa ar­dhi ya Bongo kocha kuwaponda wachezaji wake hata kama ame­pata matokeo, tofauti kwa Za­hera amekuwa akiwaponda hata kama wamepata matokeo katika mchezo wao hali ambayo imezidi kumfanya awashangaze wengi wakiamini kuwa anatengeneza chuki kwa wachezaji.

Ibrahim Ajibu ni miongoni mwa wachezaji ambao walikum­bwa na suala hili na alisema wazi kuwa licha ya wengi kuamini Ajibu anafanya vizuri bado amekuwa haonyeshi juhudi akiwa uwanjani hivyo anawakati mgumu kupata namba Taifa Stars.

Amissi Tambwe naye kocha al­isema kuwa anapenda kula ugali hali inayomfanya aongezeke uzito na kushuka kiwango chake akiwa uwanjani, ajabu hata Heri­eter Makambo ambaye ana ma­bao 7 kocha alisema kuwa hana umakini na anafikiria kumleta Mama yake(Mama Zahera) ili awe mshambuliaji kutokana na uzembe wa mchezaji huyo.

KUWEKA KAMBI MO­ROGORO

Yanga hawakufanya maan­dalizi siriazi, walikuwa na kambi ya kuungaunga mjini Morogoro huku wakubwa wenzao Simba na Azam wakienda nje.

Simba ilikuwa Uturuki na Azam ikaweka kambi Uganda.

Hali ya uchumi wa Yanga ili­kuwa ni duni, hivyo maandalizi ya kambi hiyo yaliwapa wasiwasi mkubwa mashabiki ambao ha­waamini matokeo wanayoyaona kwa sasa Jangwani.

KUVAA KOFIA

Tabia hii amekuwa nayo kwa muda mrefu kwani kila akiwa benchi hawezi kukosa kuvaa kofia hali ambayo imewafanya baadhi ya wachezaji wake kuiga mtindo huo kwa kuvaa kofia mara kwa mara.

Zahera hapendi makuu hasa kwa upande wa mavaz. Anatupia kawaida sana saa nyingine hata kipensi na tisheti anapiga anat­inga uwanjani.Ni mpenzi sana wa kofia anapokuwa kwenye benchi la ufundi.

MTU WA MAGAZETI NA TV

Anatoa ushirikiano sana kwa vyombo vya habari na hatafuni maneno. Amekuwa akijibu kwa ufasaha majibu mengi anay­oulizwa na waandishi muda wote.

Anajitahidi kuongea lugha ya kiswahili chenye lafudhi ya kikon­go ili aweze kwenda sawa na waandishi wa habari akiwa ana­waelezea jambo ambao anahitaji waweze kulitambua.

Ni mwalimu ambaye amekuwa akieleza mambo mengi yanayo­husu wachezaji na kuwakosoa wachezaji wake mbele ya vyo­mbo vya habari bila ya kupepesa macho akiwa mbele ya kamera. Anapenda sana kutumia maga­zeti kuwasiliana na mashabiki wake.

STORI: LUNYAMADIZO MLYUKA

Comments are closed.