The House of Favourite Newspapers

Mwizi wa Gari Ashambuliwa na Nyuki, Ajisalimisha Polisi

0

FRANCIS SIKADIGU anayesadikiwa kuwa aliiba gari nchini Uganda, alijisalimisha kituo cha polisi cha Bungoma nchini Kenya Jumapili iliyopita baada ya kuvamiwa na kundi la nyuki.

Polisi wa Bungoma wamesema mtu huyo alijisalimisha katika kituo hicho na kukiri kwamba alikuwa ameiba gari dogo ambapo nyuki walimvamia alipokuwa akijaribu kuondoka nalo.

 

Mtu huyo aliwashangaza watu wakati anakimbilia kituo cha polisi huku nyuki wakimfuata ambapo baadaye alikimbia kutoka kituo hicho kwenda kwa mganga wa kienyeji ili amwokoe na janga hilo.

John Wafula, mmiliki wa gari hilo, alisema mtuhumiwa huyo alimwendea akitaka kukodi magari matano hasa aina ya Toyota Premio na  Axio.

 

“Nilimwambia bei ilikuwa ni  Sh 5,000 kwa kila gari kwa siku tano,” alisema Wafula akiongeza kwamba baada ya mazungumzo hayo aliporudi mezani na kunywa juisi yake alianza kujisikia kupoteza fahamu ambapo baadaye alijikuta hospitali na kung’amua kwamba funguo za gari lake zilikuwa hazipo.

 

“Nilimwendea mganga wa kienyeji aliyenihakikishia kwamba  gari langu lingepatikana baada ya siku tatu na kwamba mwizi asingeondoka mjini Bungoma na kwamba angeshambuliwa na nyuki,” alisema Wafula.

Baada ya mtu huyo kuwaponyoka nyuki hao, alikamatwa na kufikishwa katika kituo cha polisi cha Bungoma ambapo baada ya upelelezi atafunguliwa mashitaka.

Leave A Reply