Mzungu afanya kikao na Okwi, Nyoni
WAKIREJEA uwanjani na kuanza mazoezi tangu watoke kwenye majeraha, Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Patrick Aussems, juzi alifanya kikao na mshambuliaji wake Mganda, Emmanuel Okwi na beki kiraka, Erasto Nyoni.
Wachezaji hao ambao waliukosa mchezo uliopita wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya JS Saoura ya Algeria huenda wakawa sehemu ya kikosi kitakachoivaa AS Vita mchezo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, kesho Jumamosi.
Okwi na Nyoni wote kwa pamoja wanarejea uwanjani na kuanza mazoezi baada ya kupona majeraha ya goti yaliyokuwa yanawasumbua waliyoyapata kwa nyakati tofauti.
Championi Ijumaa, lilishuhudia vikao hivyo vikifanyika kwa wakati tofauti kabla ya mazoezi kuanza juzi saa kumi jioni kwenye Uwanja wa Boko Beach Veterani, Dar.
Gazeti hili lilianza kushuhudia kikao cha kocha huyo akiwa na msaidizi wake, Denis Kitambi na Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu, na walimuita Okwi na kuanza kuzungumza.
Kikao hicho kilifanyika katikati ya uwanja ambacho kilitumia dakika saba na kikubwa walitaka kujua maendeleo ya majeraha yake kabla ya baadaye kumruhusu kwenda kujiandaa na programu ya mazoezi.
Baada ya kumalizana na Okwi, kocha huyo alimuita Nyoni na kuzungumza kabla ya dakika chache kumuita daktari mkuu wa timu hiyo, Yassin Gembe.
Daktari huyo aliitwa kwa ajili ya kuthibitisha kupona kwa Nyoni kabla ya kumjumuisha katika kikosi chake kitakachoivaa AS Vita.
Akizungumzia hilo, Aussems alisema: “Nimekutana na Okwi, Nyoni kikubwa kuzungumzia maendeleo ya majeraha yao, wapo fiti kucheza mchezo huu na AS Vita.”
Stori na Wilbert Molandi na Musa Mateja
Comments are closed.